VIGEZO NA MASHARTI YA BENKI YA I&M (I&M BANK LIMITED)
VIGEZO NA MASHARTI YA JUMLA
Kwa kuzingatia makubaliano mengine yoyote yatakayofanywa kwa maandishi kati ya Benki na Mteja, uhusiano kati ya Benki na Mteja utaongozwa na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama zitakavyokuwa zinatumika katika vipindi mbalimbali, isipokuwa pale ambapo vigezo na mashart ya jumla yafuatayo yatatumika (“Vigezo na Masharti ya Jumla”):
1. Fasili
(i) “Akaunti” maana yake ni aina yoyote ya akaunti inayomilikiwa na Mteja katika Benki (ikiwamo bila ukomo wowote) akaunti yoyote inayohusiana na karadha, amana, mkataba, bidhaa, muamala au huduma yoyote iliyoanzishwa na kuendeshwa kati ya Benki na Mteja.
(ii) “Salio lililopo” maana yake ni kiasi cha fedha kilichomo katika Akaunti ambacho Mteja anaweza kukitoa bila kuwapo kwa kizuizi chochote kutoka Benki (kiasi kinachozuiwa kinajumuisha, bila ukomo, mikopo yoyote ambayo haijathibitishwa, kiasi chochote kilichowekwa kimakosa katika Akaunti na/au kiasi chochote ambacho Benki ina haki ya kufanya makato ya fidia ya deni);
(iii) “Fomu ya Maombi” maana yake ni fomu ya Benki inayojazwa na Mteja kwa madhumuni ya kufungua na kuendesha Akaunti.
(iv) “Mtia Saini Aliyeidhinishwa” maana yake ni Mteja na/au kuhusiana na Mteja, mtu au watu walioteuliwa na kuidhinishwa kwa maandishi na Mteja wa Benki kuendesha Akaunti kwa niaba ya Mteja.
(v) “Benki” maana yake ni I & M Bank (T) Limited, ikijumuisha, bila ukomo, warithi wake wa kisheria na waliokabidhiwa haki au majukumu (iwe ni kwa uasili wake au kwa kupitishwa).
(vi) “Matawi ya Benki” maana yake ni (ikiwamo ofisi kuu iliyosajiliwa ya Benki) maeneo yote, ndani au nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambapo shughuli za Benki zinaendeshwa.
(vii) “Siku ya Kazi” maana yake ni siku yoyote ambayo Benki iko wazi kwa shughuli zote za kibenki (isipokuwa siku za mapumziko zinazotambulika kisheria na siku za mapumziko ya umma), kama Benki itakavyoainisha katika vipindi mbalimbali.
(viii) “Saa za Kazi za Benki” maana yake ni saa ambazo Benki huwa wazi kama kawaida kwa ajili ya shughuli zote za kibenki, kama zitakavyoamuliwa na Benki kwa kila tawi lake katika vipindi mbalimbali.
(ix) “Ada za Benki” maana yake ni (ikiwa ni pamoja na japo si hizi tu) jedwali la tozo na ada zinazotozwa na Benki kuhusiana na Akaunti.
(x) “Hundi” maana yake ni fomu za hundi zinazotolewa na Benki kwa Mteja na ambazo ni sehemu ya Kitabu cha Hundi.
(xi) “Kitabu cha Hundi” maana yake ni hundi zilizo na namba za mfuatano, zilizounganishwa pamoja na kutolewa na Benki kwa Mteja.
(xii) “Vigezo na Masharti ya Kitabu cha Hundi” maana yake ni Vigezo na Masharti Mahususi yanayohusu matumizi ya Mteja ya Hundi na Kitabu cha Hundi.
(xiii) “Mteja” maana yake ni mmiliki wa Akaunti.
(xiv) “Deni” maana yake ni fedha zote, wajibu na dhima za aina yoyote, iwe ni mtaji, riba au vinginevyo, katika Shilingi za Tanzania au Fedha za Kigeni, ambazo Mteja anaweza kutakiwa, kudaiwa au kuwajibika kwa Benki, iwe sasa au baadaye, halisi au dharura.
(xv) “Fedha za Kigeni” maana yake ni fedha zozote, kwa jina au mfumo wowote, isipokuwa Shilingi ya Tanzania.
(xvi) “Shilingi ya Tanzania
” maana yake ni fedha halali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
(xvii) “Mamlaka” maana yake ni utaratibu wa uendeshaji wa Akaunti kama ulivyobainishwa na Mteja katika Fomu ya Maombi; (xviii) “Dhamana” maana yake ni (ikiwamo japo si haya tu) makubaliano yoyote, rehani, dhamana ya mali, amana, haki ya zuio, udhamini, fidia, hatifungani na/au dhamana nyingine yoyote inayohakikisha, kwa sehemu au kwa ukamilifu Deni lolote la Mteja kwa Benki;
(xix) “Vigezo na Masharti Mahususi” maana yake ni vigezo na masharti yanayohusiana na aina maalumu ya Akaunti; na
(xx) “Kodi” maana yake ni kodi zote, tozo, ushuru, ada, makato au malipo ya lazima (ikiwamo, bila ukomo, kodi za kifedha, kikanuni, kisheria, za manispaa au nyinginezo), pamoja na faini, tozo na riba zote zinazohusiana nazo.
2. Ustahiki
Benki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, baada ya kupokea maombi sahihi kutoka kwa Mteja na kwa kuzingatia Vigezo na Masharti ya Jumla pamoja na Vigezo na Masharti Mahususi yanayohusu Akaunti inayohusika, inaweza kufungua Akaunti kwa ajili ya Mteja. Benki haitafungua Akaunti kwa ajili ya Mteja yeyote ambaye jina lake limo katika orodha yoyote ya watu waliopigwa marufuku (iwe ya ndani au ya kimataifa) inayotolewa, kusambazwa au kupatikana kwa Benki katika vipindi mbalimbali.
3. Anwani ya Mteja
Anwani iliyotajwa na Mteja katika Fomu ya Maombi itachukuliwa na Benki kuwa ndiyo anwani rasmi ya Mteja, na mawasiliano yote ya maandishi yatatumwa na Benki kwenda kwenye anwani hiyo. Mteja anatakiwa kuijulisha Benki kwa maandishi kuhusu mabadiliko yoyote ya anwani hiyo.
4. Jina la Mteja
Akaunti itaendeshwa na Mteja kwa jina au majina yaliyoainishwa katika Fomu ya Maombi na nyaraka zote zinazohusiana nayo. Benki ina haki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, kumtaka Mteja awasilishe uthibitisho wowote unaohitajika kuhusu jina lake na mabadiliko yoyote ya jina hilo, na Benki itakuwa huru kukataa kutekeleza maelekezo yoyote ya Mteja hadi pale ambapo maombi hayo yatakapoiridhisha Benki kikamilifu.
5. Taarifa za Mteja
Benki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, wakati wowote katika kipindi chote cha uendeshaji wa Akaunti, ina haki ya kumtaka Mteja awasilishe taarifa na/au nyaraka zozote ambazo Benki itaona ni muhimu kwa ajili ya kufungua na/au kuendesha Akaunti.
6. Maelekezo ya Mteja
(i) Benki itawajibika kutekeleza tu maelekezo halisi ya awali ya Mteja yaliyoidhinishwa ipasavyo na/au nyaraka zilizotolewa au kukubaliwa kwa mujibu wa Mamlaka, hadi pale Mteja atakapotoa notisi ya maandishi kwa Benki ya kubadili hali hiyo.
(ii) Maelekezo yatakayopokewa baada ya Saa za Kazi za Benki au katika Siku isiyo ya Kazi yatashughulikiwa katika Siku ya Kazi inayofuata. Mteja anaweza kufuta maelekezo mradi tu Benki haijafungwa kisheria kutekeleza maelekezo hayo na kwa sharti la ziada kwamba Benki imethibitisha kwa maandishi kuwa maelekezo hayo bado hayajatekelezwa. Benki itakuwa na haki ya kutoza ada kwa mujibu wa Ada za Benki kwa kufuta maelekezo.
(iii) Benki, kwa kuzingatia masharti ambayo itaona yanafaa kwa hiari yake kamili na ya pekee, na baada ya kupokea maombi ya maandishi kutoka kwa Mteja, inaweza kutekeleza maelekezo ya mdomo, kwa njia ya faksi, kwa njia za kielektroniki au kwa aina nyingine zozote za mawasiliano yasiyo ya maandishi. Hata hivyo, Benki haitawajibika, na Mteja ataifidia na kuilinda Benki dhidi ya hasara yoyote, iwapo Benki itatekeleza maelekezo yaliyopotoshwa au kutumwa isivyo sahihi, au endapo taarifa zilizomo katika mawasiliano hayo hazitapokewa au zitachelewa kufika.
(iv) Benki inaweza kukataa kutekeleza maelekezo ya Mteja endapo maelekezo hayo hayako wazi na/au endapo Benki ina sababu ya kuamini kuwa Mteja hakutoa maelekezo hayo, na/au endapo Benki itaona kuwa utekelezaji wa maelekezo hayo unaweza kusababisha ukiukwaji wa sheria, kanuni, mwongozo au wajibu mwingine wowote unaoitaka Benki kuuzingatia.
7. Saini Sampuli
Mteja atawasilisha Benki, kwa namna inayokubaliwa na Benki kwa hiari yake kamili na ya pekee, sampuli ya saini ya kila Mtia saini Aliyeidhinishwa. Benki inaweza kuhitaji sampuli mpya ya saini endapo kutakuwa na mabadiliko ya jina la Mteja.
8. Amana na Mikopo
(i) Mteja anaweza kuweka kwenye Akaunti fedha taslimu, hundi na/au hati nyinginezo kwa ajili ya kuingizwa kama mkopo katika Akaunti, kwa namna na katika fomu itakayokubalika kwa Benki. Benki haitawajibika kuhusu fedha taslimu zitakazotumwa kwa njia ya posta. Hundi na/au hati nyinginezo zote zitakazotumwa kwa njia ya posta zitapaswa kuwekwe alama ya
“Account Payee Only/Not Negotiable” na lazima malipo yafanyike kwa jina la Akaunti ya Mteja.
(ii) Hati yoyote, iwe inahamishika au isiyohamishika, ya aina yoyote ile, itakubaliwa na Benki kwa ajili ya kuwekwa au kukusanywa kwa dhamana ya Mteja mwenyewe. Benki, bila kutoa taarifa ya awali, ina haki ya kubatilisha miamala yoyote katika Akaunti na kutoza kiasi chochote kilichoingizwa kama mkopo kuhusiana na hati za ahadi ya malipo, hawala za fedha, hundi au hati nyinginezo zilizoingizwa katika Akaunti ambazo baadaye zitarudishwa bila kulipwa kwa sababu yoyote ile, iwe Benki ilimjulisha Mteja au vinginevyo kuhusu miamala na mikopo hiyo. Kubatilisha miamala na kutoza kiasi hicho hakuathiri haki ya Benki ya kuhifadhi hati hizo ambazo hazijalipwa na kutumia kwa manufaa yake haki zote zinazohusiana na hati hizo.
(iii) Benki haitachukua jukumu lolote wala kuwajibika kwa thamani itakayowekwa kwa fedha na mlengwa au benki mshirika, mradi tu Benki imetekeleza maelekezo ya Mteja.
(iv) Benki hufanya kazi kama wakala wa makusanyo wa Mteja pekee, na haitachukua jukumu lolote katika utekelezaji au ufanikishaji wa hati zozote zilizowekwa Benki kwa ajili ya kukusanywa; na
(v) Majadiliano na ukusanyaji wa hati zinazoweza kuhamishwa zilizoainishwa katika Fedha za Kigeni, yatakuwa chini ya Kanuni za Chama cha Kimataifa cha Wafanyabiashara kama zilivyo sasa au kama zitakavyorekebishwa na/au kubadilishwa hapo baadaye.
9. Malipo ya Fedha
(i) Benki itamlipa Mteja kwa fedha baada ya kuwasilishwa kwa hundi iliyosainiwa ipasavyo na Mtia Saini Aliyeidhinishwa tu.
(ii) Pale ambapo hundi itawasilishwa na mtu mwingine yeyote mbali na Mteja kwa ajili ya malipo ya fedha, Benki inaweza kuhitaji uthibitisho kutoka kwa Mtia Saini Aliyeidhinishwa kabla ya kufanya malipo kwa mtu huyo; na
(iii) Pale ambapo Mtia Saini Aliyeidhinishwa ataiomba Benki kufanya malipo kwa mujibu wa kifungu kidogo (ii) hapo juu, Mteja ataifidia Benki kikamilifu na bila masharti yoyote kwa malipo yote yatakayofanywa na mwenye hundi, iwe fedha hizo zitapokewa na Mteja au vinginevyo, na iwe maelekezo ya malipo ni maelekezo halisi ya Mteja au vinginevyo.
10. Utoaji wa Fedha na Malipo
(i) Kwa kuzingatia kikomo cha kila siku cha utoaji fedha (kama kipo), Salio Lililopo linalotosheleza na Vigezo na Masharti Mahususi ya Akaunti, Mteja anaweza kutoa fedha na/au kufanya malipo kutoka katika Akaunti.
(ii) Mteja hataruhusiwa kutoa fedha kinyume, na Benki haitalazimika kufanya malipo kinyume na hundi au malipo mengine ambayo hayajathibitishwa.
11. Maombi ya Fedha kwa Wakati Mmoja
Endapo Benki itapokea maelekzo kadhaa kutoka kwa Mteja kwa ajili ya utoaji na/au malipo kutoka katika Akaunti kwa takribani wakati mmoja, kiasi kwamba jumla ya kiasi kinachoombwa kuzidi Salio Lililopo, Benki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, inaweza kutekeleza baadhi ya maelekezo hayo kwa mpangilio na/au kwa namna itakayoona inafaa.
12. Tozo na Gharama za Benki
(i) Benki itakuwa na haki ya kulipwa na Mteja, na itakuwa huru kutoza Akaunti kwa:
(ii) gharama zote ambazo Benki itatumia na katika kushughulikia au kujaribu kushughulikia hundi au malipo mengine yoyote yatakayoingizwa katika Akaunti ya Mteja;
(iii) riba (ikiwamo riba ya ucheleweshaji na/au riba ya ziada, endapo itakuwapo) kwenye Akaunti iliyotolewa zaidi salio, akaunti ya mkopo au nyinginezo.
(iv) huduma nyingine yoyote ya mkopo iliyotolewa na Benki kwenda kwa Mteja, kwa kiwango cha riba cha mwaka na kwa njia ya kuhesabu na kujumlisha riba kama itakavyoamuliwa na Benki kwa hiari yake kamili, bila kutoa taarifa kwa Mteja (kwa kuzingatia mipaka inayoruhusiwa kisheria);
(v) ada za kisheria na/au kitaaluma, pale inapohitajika, kwa misingi ya wakili/mteja, zitakazotumika na Benki katika kupata ushauri wowote wa kisheria na/au kitaaluma unaohusiana na Akaunti, maandalizi ya nyaraka zozote zinazohusu huduma ya mkopo ya Mteja na/au miamala yoyote ya Mteja na Benki;
(vi) ada za ushughulikiaji, ada za ahadi za mikopo, kamisheni na ada nyinginezo, kwa viwango, nyakati na kwa namna ambayo Benki itaamua katika vipindi mbalimbali; na
(vii) gharama na tozo zote nyingine zinazotozwa na Benki kama zilivyoainishwa kwa kina katika Ada za Benki (nakala yake inapatikana kwa maombi).
13. Taarifa za Akaunti
(i) Benki itampatia Mteja taarifa ya Akaunti mara kwa mara ikionesha miamala yote iliyofanyika katika Akaunti. Benki inaweza pia (kwa maombi ya maandishi ya Mteja na baada ya kulipwa kwa ada inayohusika) kumpatia Mteja taarifa za ziada na/au kutoa taarifa kwa vipindi vitakavyokubaliwa kati ya Benki na Mteja; na
(ii) Maudhui ya taarifa yoyote iliyotolewa na Benki kwa Mteja ambayo Mteja hajapinga ndani ya siku ishirini na nane (28) tangu kupokewa kwake, yatachukuliwa kuwa yamekubaliwa na Mteja na, pasipo kuwapo kosa lililo wazi, yatakuwa uthibitisho kamili wa miamala yote iliyofanyika katika Akaunti na hayataweza kupingwa na Mteja kwa sababu yoyote ile;
(iii) Kwa madhumuni yote, ikiwamo mashauri ya kisheria, cheti kilichosainiwa na mkurugenzi yeyote, meneja na/au Mtia Saini Aliyeidhinishwa wa Benki kuhusu jambo lolote linalohusiana na Akaunti na/au Deni lolote, pasipo kuwapo kosa lililo wazi, kitakuwa uthibitisho kamili dhidi ya Mteja kuhusiana na jambo hilo na/au deni linalohusika.
14. Malipo ya Kawaida/Makato ya Moja kwa Moja
Benki inaweza kumruhusu Mteja kufanya makato au utoaji wa fedha wa moja kwa moja kwa njia ya kiotomati (kama vile Makato ya Moja kwa Moja au Malipo ya Kawaida) kutoka katika Akaunti, isipokuwa kama Vigezo na Masharti Mahususi ya Akaunti yanasema vinginevyo. Miamala yote hiyo itatekelezwa kwa hiari ya Benki, na Benki ina haki ya kutotekeleza maelekezo yoyote yanayohusiana na Makato ya Moja kwa Moja au Malipo ya Kawaida pale ambapo Salio Lililopo halitakuwa linalotosheleza.
15. Makosa ya Uhasibu na Uwasilishaji
(i) Benki, bila kutoa taarifa ya awali kwa Mteja, ina haki ya kutoza kiasi chochote kilichoingizwa kimakosa katika Akaunti na/au kubatilisha maingizo yoyote yaliyofanywa kimakosa katika Akaunti. Benki haitawajibika kwa athari zozote zitakazotokana na kutoza na/au kubatilisha maingizo hayo. Kiasi chochote kilichoingizwa kimakosa na Benki katika Akaunti na kutumiwa na Mteja kitapaswa kilipwe haraka kwa Benki, pamoja na riba zote zinazohusika zilizopatikana, ndani ya saa ishirini na nne (24) tangu Benki ilipowasilisha madai ya malipo hayo kwa Mteja.
(ii) Maelekezo ya malipo, miamala ya ubadilishaji fedha, pamoja na ununuzi na uuzaji wa dhamana nchini Tanzania au kwingineko, yanayotekelezwa na Benki kwa niaba ya Mteja, yatafanywa kwa gharama ya Mteja mwenyewe. Benki, washirika wa benki, wafanyakazi wake, hawatawajibika kwa dosari, upotoshaji au upungufu wowote (ikiwamo japo bila ukomo, mifumo ya nyaya, usafiri wa anga, huduma za usafirishaji wa haraka, baruapepe, teleksi au faksi) utakaojitokeza kwa namna yoyote ile.
16. Riba
(i) Riba italipwa tu kwa salio la mkopo lililopo katika Akaunti inayozalisha riba. Riba itahesabiwa kwa kiwango ambacho Benki itaamua na kubadilisha katika vipindi mbalimbali.
(ii) Riba italipwa na kuingizwa katika Akaunti kwa namna ilivyoainishwa katika Vigezo na Masharti na Mahususi ya Akaunti; na
(iii) Riba itahesabiwa kwa jumla, na Kodi yoyote ambayo Benki inatakiwa kulipa itakatwa kutoka katika Akaunti.
17. Huduma ya Mikopo Iliyowekwa na Benki kwa Ajili ya Mteja
Baada ya Mteja kuwasilisha maombi sahihi, Benki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, inaweza kumpatia Mteja huduma ya mkopo, na itakuwa na haki ya kutoza Akaunti kwa riba zote, kamisheni, gharama, matumizi na tozo nyinginezo (ikiwamo tozo za kibenki na kisheria) zitakazotumika kuhusiana na utoaji wa huduma hiyo ya mkopo.
18. Urejeshaji wa Fedha Zilizotolewa Zaidi katika Akaunti
(i) Mteja hatakiwi kutoa fedha katika Akaunti kinyume na kiwango cha chini kilichoainishwa kwa Akaunti inayohusika (au kuzidisha kiwango cha ukomo cha mkopo wa ziada kilichotolewa na kuidhinishwa na Benki kwa Akaunti hiyo) bila ridhaa ya maandishi ya awali ya Benki. Benki itakuwa huru, kwa hiari yake kamili na ya pekee, kukataa hundi, kufanya malipo na/au kuruhusu utoaji wa fedha endapo athari yake itakuwa ni kutoa kiasi cha Akaunti zaidi ya kiwango cha chini cha salio lililoainishwa au kuzidisha kiwango cha ukomo kilichoidhinishwa; na
(ii) Endapo Akaunti itatolewa zaidi ya kiwango cha chini cha salio kilichoainishwa au kuzidisha kiwango cha ukomo kilichoidhinishwa bila ridhaa ya maandishi ya awali ya Benki, Mteja atalipa (ikiwamo bila ukomo) ada zitakazoainishwa na Benki pamoja na riba ya ziada kwa kiasi kinachohusika cha kiwango cha chini cha salio au kiasi kilichozidi ukomo kilichoidhinishwa (katika kifungu hiki vinajulikana kwa pamoja kama
“kiasi kinachodaiwa
”), kwa kiwango au viwango na kwa njia ya kuhesabu na kujumlisha riba kama itakavyoamuliwa na Benki kwa hiari yake kamili, hadi kiasi hicho kitakapolipwa kikamilifu. Benki pia itakuwa huru kudai kutoka kwa Mteja urejeshaji wa haraka na kamili wa kiasi chote kinachodaiwa, pamoja na riba yote iliyopatikana juu yake na gharama, tozo na matumizi mengine yote yanayotokana na hali hiyo.
19. Haki ya Zuio ya Benki
(i) Endapo kutakuwa na Deni, Benki itakuwa na haki ya kuweka zuio la jumla kuhusu mali zote za Mteja zilizo katika umiliki wa Benki, ikiwamo (bila ukomo) fedha, bidhaa, dhamana au vitu vya thamani vinavyoshikiliwa na Benki, hundi zilizowasilishwa kwa ajili ya malipo, amana na mali nyingine yoyote (inayohamishika au isiyohamishika) iliyowekwa rehani au kudhaminiwa kwa namna yoyote na Mteja kwa manufaa ya Benki ili kuhakikisha urejeshaji wa Deni; na
(ii) Benki, wakati wowote, iinaweza kumpa Mteja notisi ya maandishi kwamba iwapo Deni halitalipwa ndani ya muda uliobainishwa, Benki, bila notisi nyingine yoyote kwa Mteja, inaweza kutekeleza haki na hatua zake zozote chini ya Dhamana yoyote ili kurejesha Deni hilo.
20. Haki ya Benki ya Kulipwa Deni
(i) Shughuli zote kati ya Benki na Mteja, za aina yoyote ile, zitachukuliwa na Benki kwa madhumuni yote kuwa ni akaunti moja iliyounganishwa, isiyotenganishwa wala kugawanyika, na Benki:
(ii) Bila kutoa notisi, inaweza kutumia salio lolote la mkopo lililopo katika Akaunti (iwe ni akaunti ya hundi, ya mkopo, ya akiba, ya amana ya muda au aina nyingine yoyote ya akaunti, au katika akaunti ya mtu mwingine yeyote ambaye Mteja amekubali kumdhamini) kulipa Deni lolote linalodaiwa na Benki kutoka kwa Mteja au mtu mwingine yeyote ambaye Mteja amekubali kuwa mdhamini wake. Haki hii ya kulipwa deni kwa salio itaongezeka juu yake, na haitapunguza wala kuathiri, haki nyingine zozote za Benki za kurejesha madeni;
(iii) Kubadilisha, kwa viwango vya ubadilishaji vya Benki vinavyotumika wakati huo, fedha zozote zinazoshikiliwa na Benki katika Fedha za Kigeni ambazo ziko chini ya haki ya zuio ya Benki, na kisha kutekeleza haki ya Benki ya Kulipwa Deni kwa Kutumia Salio. Benki haitawajibika kwa hasara yoyote itakayosababishwa na ubadilishaji huo wa fedha; na
(iv) Kulipa deni kwa amana ya muda (ikiwamo ile iliyowekwa katika Fedha za Kigeni na/au kwa kipindi maalumu) na kutekeleza haki ya Benki ya Kulipwa Deni kwa Kutumia Salio, hata kama muda wa amana hiyo haujaisha au riba haijapatikana.
21. Mabadiliko ya Uhusiano na Kufungwa kwa Akaunti
(i) Mteja, baada ya kutoa kwa Benki notisi ya maandishi ya siku thelathini (30) au notisi nyingine kama Benki itakavyoona inafaa, anaweza kufunga Akaunti, kwa sharti la kulipwa kwa Deni lolote lililopo;
(ii) Benki inaweza wakati wowote, baada ya kumpa Mteja notisi, kusitisha au kubadilisha uhusiano wake wa kibiashara na Mteja na/au kufunga Akaunti, na inaweza kumtaka Mteja kulipa Deni lolote litakalotokana na uamuzi, mabadiliko na/au kufungwa huko; na
(iii) Endapo Benki itasitisha au kubadilisha uhusiano wake na Mteja na/au kufunga Akaunti, itakuwa ni jukumu la Mteja peke yake kuwajulisha wahusika wengine wowote kuhusu kusitishwa, kubadilishwa na/au kufungwa huko.
22. Kufungiwa Akaunti
Benki, kwa hiari yake kamili, inaweza wakati wowote kukataa kupokea au kutekeleza maelekezo yoyote yanayohusiana na Akaunti, kwa muda wote ambapo:
- kuna mgogoro wowote kati ya Mteja na Benki; au
- Benki ina sababu yoyote ya kushuku kuwa udanganyifu umefanyika au una uwezekano wa kufanyika; au
- Akaunti inatumika au ina uwezekano wa kutumiwa na Mteja kwa miamala isiyo halali na/au kinyume cha sheria; au
- Benki ina shaka, kwa sababu yoyote ile, kwamba ama Mteja si mtu anayestahili kuendesha Akaunti au kuna mgogoro wowote kuhusiana na Mamlaka; au
- Benki iko chini ya wajibu wa kisheria kufanya hivyo.
23. Kitabu cha Hundi
(i) Kitabu cha Hundi kitatolewa na Benki kwa Mteja kwa hiari ya Benki pekee, kwa kuzingatia Vigezo na Masharti ya Kitabu cha Hundi yaliyobainishwa katika kifungu hiki na yaliyochapishwa ndani ya jalada la Kitabu cha Hundi.
(ii) Benki inaweza kutoza ada kwa ajili ya utoaji wa Kitabu cha Hundi na Kitabu chochote cha ziada cha Hundi kitakachotolewa kwa Mteja.
(iii) Benki inaweza kukataa kufanya malipo kwa Mteja au mtu mwingine yeyote kwa hundi yoyote ambayo haijaandaliwa kwa mujibu wa Vigezo na Masharti ya Kitabu cha Hundi yaliyoainishwa hapa chini:
(iv) Mteja anapaswa aandike, aweke tarehe na atie saini hundi kwa maandishi yaliyo wazi, kwa kutumia wino unaosomeka (ikiwezekana wa buluu au mweusi), katika fedha ya Akaunti, kwa kiasi kisichozidi Salio Lililopo.
(v) Wakati wa kuandika Hundi:
(vi) kiasi kinapaswa kioneshwe kwa maneno na kwa tarakimu, kwa namna itakayozuia kuongezwa kwa neno au tarakimu nyingine yoyote na/au kuzuia mabadiliko ya udanganyifu.
(vii) Hundi inapaswa isainiwe na Mtia Saini Aliyeidhinishwa kwa mujibu wa masharti ya Mamlaka.
(viii) mabadiliko yoyote kwenye Hundi yanapaswa yatiwe saini na Mtia Saini Aliyeidhinishwa kwa ajili ya uthibitisho kwa mujibu wa masharti ya Mamlaka.
(ix) kuondolewa kokote kwa mistari ya Hundi kunapaswa kufanywe na Mtia Saini Aliyeidhinishwa kwa mujibu wa masharti ya Mamlaka.
(x) hakuna Hundi isiyokamilika itakayotolewa kwa mtu yeyote; na
(xi) Hundi zote ambazo hazijakamilishwa zinapaswa zihifadhiwe mahali salama wakati wote.
(xii) Mteja anapaswa ahesabu idadi ya Hundi zilizomo katika Kitabu cha Hundi wakati wa kupokea Kitabu hicho na wakati wote wa matumizi yake. Endapo Hundi yoyote itabainika kupotea au kukosekana, Mteja anapaswa kuijulisha Benki haraka.
(xiii) Benki inaweza kukataa kupokea Hundi endapo tarehe ya hundi ni zaidi ya miezi sita (6) iliyopita au endapo tarehe ya Hundi ni ya siku zijazo.
(xiv) endapo Mteja atataka Benki isimamishe malipo ya Hundi, atapaswa aiombe kwa maandishi haraka ili itekeleze kusudi lake hilo. Baada ya kupokea notisi ya maandishi ya kusimamisha malipo ya hundi kutoka kwa Mteja,
(xv) Benki itainakili notisi hiyo na kusimamisha malipo mradi notisi hiyo imepokewa kabla ya muamala unaotakiwa kusimamishwa haujafanyika. Benki inabaki na haki ya kutoza ada za kiuendeshaji kwa kusimamisha malipo ya Hundi.
(xvi) Benki haitawajibika kwa namna yoyote kwa Mteja, na Mteja ataifidia Benki kikamilifu dhidi ya madai yoyote ya mtu mwingine endapo Benki itafanya malipo kwa niaba ya Mteja kupitia Hundi ambayo inadhaniwa kuwa imetolewa na Mteja, lakini saini au maudhui ya Hundi hiyo na/au maelekezo ya maandishi yameghushiwa, iwapo:
- Mteja amechangia au kuwezesha kughushi huko; au
- kumekuwapo na kughushi hapo awali kwa Hundi ya Mteja au hati ya maelekezo bila Mteja kupinga malipo hayo hapo awali,
(xvii) Benki hufanya kazi kama wakala wa ukusanyaji wa Mteja pekee, na endapo Hundi ya Mteja au hati nyingine yoyote ya mtu mwingine itapotea au kuibwa ikiwa chini ya usimamizi wa Benki, Benki haitawajibika kwa hasara yoyote ya faida au fursa itakayompata Mteja au mtu mwingine yeyote na/au kwa ada zozote zitakazotumika kwa Mteja au mtu mwingine yeyote katika kusimamisha malipo ya hati hiyo, hata pale ambapo Benki imekuwa na uzembe.
24. Akaunti za Pamoja
Vigezo na Masharti Mahususi yafuatayo yatatumika katika Akaunti za Pamoja:
(i) pale ambapo Akaunti ya Pamoja inaendeshwa chini ya Mamlaka iliyoainishwa kwa Kiingereza kama
‘Either/or Survivor’: kila Mteja wa Akaunti ya Pamoja anaidhinishwa kuendesha Akaunti ya Pamoja peke yake, na itachukuliwa kuwa maelekezo yanayotolewa na Mteja mmoja kwenye Akaunti ya Pamoja yameidhinishwa na Mteja/Wateja wengine wa Akaunti ya Pamoja.
(ii) pale Akaunti ya Pamoja inapoendeshwa chini ya Mamlaka iliyoainishwa kwa lugha ya Kiingereza kama
‘Jointly’: kila Mteja wa Akaunti ya Pamoja anaidhinishwa kuendesha Akaunti ya Pamoja akiwa tu pamoja na wateja wengine wote wa Akaunti ya Pamoja (au kama ilivyobainishwa katika Mamlaka). Benki haitawajibishwa kwa kukataa kutekeleza maelekezo au kwa kuchelewa kukubali maelekezo ambayo hayajatolewa na Wateja wote wa Akaunti ya Pamoja.
(iii) endapo Mteja yeyote wa Akaunti ya Pamoja atatoa maelekezo yanayopingana, au yanayoonekana kupingana, na maelekezo yaliyotolewa na Mteja/Mateja wengine wa Akaunti ya Pamoja, Benki inaweza kukataa kutekeleza maelekezo hayo hadi mgongano huo utakapotatuliwa kwa namna itakayoiridhisha Benki pasipo kuwa na shaka; na
(iv) kila Mteja wa Akaunti ya Pamoja atawajibika kwa pamoja na kila mmoja kulipa Deni lolote linalohusiana na Akaunti ya Pamoja.
25. Amana ya Kudumu
Benki, kwa hiari yake pekee, inaweza kupokea fedha katika fedha maalumu kutoka kwa Mteja ili ziwekwe katika Akaunti ya amana inayozalisha riba kwa kipindi maalumu. Vigezo na Masharti Mahususi yatakayoainishwa na Benki kuhusiana na Akaunti hizo yatatumika, na endapo kutakuwa na tofauti kati ya Vigezo na Masharti haya ya Jumla na Vigezo na Masharti hayo Mahususi, Vigezo na Masharti Mahususi yatatumika.
26. Akaunti za Fedha za Kigeni
Kwa kuzingatia kanuni zozote za ubadilishaji fedha (pale zinapohusika):
(i) Benki inaweza kuendesha Akaunti katika Fedha za Kigeni.
(ii) Benki, kwa maombi ya Mteja, inaweza kuingiza au kutoza Akaunti kwa fedha ambayo si fedha iliyoainishwa kwa Akaunti hiyo, na inaweza kubadilisha kiasi hicho kilichotozwa au kuingizwa kwa kiwango cha ubadilishaji kinachotumika Benki wakati huo; na
(iii) Akaunti ya Fedha za Kigeni itaendeshwa na Mteja kwa dhamana ya Mteja mwenyewe, ikijumuisha (bila ukomo) madhara ya hatua zozote za kisheria, kikodi au nyinginezo zitakazoathiri Akaunti ya Fedha za Kigeni.
27. Akaunti Zisizo Hai
(i) Akaunti itachukuliwa kuwa si hai pale itakapobaki bila kuendeshwa kwa kipindi kitakachoainishwa katika Vigezo na Masharti Mahususi ya Akaunti au kama Benki itakavyoamua katika vipindi mbalimbali; na
(ii) Benki inaweza (ikiwamo bila ukomo) kuhusisha sharti moja au zaidi kati ya masharti yafuatayo kwa Akaunti itakapopangwa kuwa isiyo hai:
- kuthibitisha uhalali na ukweli wa muamala wa kwanza wa kuihuisha Akaunti;
- kusitisha ulipaji wa riba (pale inapohusika);
- kusitisha utoaji wa Taarifa za Akaunti; na
- kutoza ada ya matengenezo kama itakavyoamuliwa na Benki katika vipindi mbalimbali.
28. Makato
Malipo yote yanayotakiwa kufanywa na Mteja kwenda Benki kwa mujibu wa Vigezo na Masharti haya ya Jumla au vinginevyo, yatafanywa kwa fedha zinazopatikana haraka bila haki ya benki ya kukata fedha, dai la kupinga au makato ya Kodi ya aina yoyote, isipokuwa pale sheria inapohitaji; ambapo, katika hali hiyo, Mteja atalipa kwa Benki kwa wakati huohuo anapofanya malipo yanayohusika, kiasi cha ziada kitakachohakikisha kwamba Benki inapokea kiasi kamili ambacho vinginevyo kingeweza kupokewa na Benki.
29. Malalamiko
Benki inaweza kuhitaji kwamba malalamiko yoyote yanayotolewa na Mteja kuhusiana na Akaunti yawe kwa maandishi. Benki itashughulikia malalamiko hayo haraka iwezekanavyo kwa namna inayokubalika, baada ya kupokea malalamiko.
30. Uwajibikaji
(i) Benki haitawajibika kwa Mteja kwa:
(a) hasara yoyote ya faida au fursa au matokeo ya hasara yoyote au dosari yoyote ya sifa ya Mteja. Benki haitawajibika kwa namna yoyote kwa Mteja au mtu mwingine kwa kufanya malipo kwa niaba ya Mteja au kwa kutekeleza maelekezo yoyote ya maandishi yanayodhaniwa kuwa yametolewa na Mteja hata kwa uzembe, iwapo saini au maudhui ya maelekezo ya maandishi yameghushiwa, endapo Mteja amesaidia kughushi huko na/au endapo kumewahi kuwapo kwa kughushi hapo awali kwa hundi ya Mteja au hati ya maelekezo ambayo Mteja hajawahi kupinga hapo awali, na/au endapo Benki imechukua tahadhari stahiki na kutenda kwa nia njema katika kufanya malipo hayo;
(b) kutenda au kutotenda kokote, ikiwamo uvunjaji wowote wa wajibu wake chini ya Vigezo na Masharti haya ya Jumla, kunakosababishwa na mazingira yaliyo nje ya udhibiti wa kawaida na wa msingi, ikiwamo (bila ukomo) moto, mgomo, uasi au ghasia, vikwazo vya kibiashara, ugaidi au vitendo vya maadui, ucheleweshaji wa usafirishaji, au matakwa au kanuni za mamlaka yoyote ya kiraia au kijeshi. Hata hivyo, kwa masuala kama wizi na uvunjaji, Benki itawajulisha wateja walioathirika haraka iwezekanavyo mradi tu kanuni za usiri hazitakiukwa na hatua hiyo haitaingilia uchunguzi wa ndani na/au wa polisi;
(c) (pale ambapo Benki inaendesha Akaunti kwa kutumia kifurushi cha programu au mfumo mwingine wa uhasibu) kushindwa kufanya kazi kwa programu hiyo kunakotokea moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja kutokana na (ikiwamo bila ukomo) mabadiliko mabaya ya umeme au uharibifu unaotokana na moto, maji, ajali, kumwagika kwa vimiminiko, kuunganisha kwenye umeme usio sahihi, nyaya za umeme zenye hitilafu au zisizo sahihi, au muunganisho usio sahihi.
(ii) Kwa kuzingatia Vigezo na Masharti haya ya Jumla, pale ambapo Benki itabainika kuwajibika kwa Mteja kwa hasara, madhara au dosari zinazotokana na ucheleweshaji au kosa la makusudi au la uzembe katika kutekeleza maelekezo ya Mteja yaliyo wazi na yasiyo na utata, dhima ya Benki itakuwa kiasi cha chini kati ya:
- kiasi cha hasara, madhara au dosari hizo; au
- kiasi cha riba ambayo Mteja hakupokea, au riba ambayo Mteja analazimika kulipa kutokana na kushindwa, ucheleweshaji au kosa hilo.
31. Uhalali wa Nyaraka
(i) Benki haiwajibiki kwa ukweli, uhalali wa kisheria, usahihi wa taratibu au thamani ya nyaraka, ikiwamo (bila ukomo) hati za mizigo, maagizo ya utoaji, nyaraka za usafirishaji, stakabadhi, waranti na hati za bima.
32. Mawasiliano
(i) Mawasiliano yoyote ya maandishi kutoka kwa Benki kwenda kwa Mteja, ikiwamo (bila ukomo) notisi yoyote inayotolewa kwa mujibu wa Vigezo na Masharti haya ya Jumla, yatachukuliwa kuwa yamepokewa na Mteja:
- endapo itakabidhiwa kwa mtu, katika tarehe na saa ya kukabidhiwa;
- endapo itatumwa kwa posta, siku ya nne tangu tarehe ya kutumwa;
- endapo itatumwa kwa barua inayosafirishwa kwa ndege, siku ya saba tangu tarehe ya kutumwa;
- endapo itatumwa kwa teleksi, pale jibu sahihi la kuthibitisha litakapopokewa;
- endapo itatumwa kwa SWIFT, pale ujumbe wa SWIFT uliothibitishwa kupokewa utakapopokewa;
- endapo itatumwa kwa faksi, baada ya kukamilika kwa uwasilishaji;
- endapo itatumwa kwa baruapepe au ujumbe mfupi wa maandishi, iwapo itatumwa kwenda kwenye anwani sahihi ya baruapepe au namba ya simu ya mkononi kama ilivyotajwa na Mteja katika Fomu ya Maombi au kama Mteja alivyoijulisha Benki katika vipindi mbalimbali; na, kwa upande wa utumaji kwa posta, itatosha kuthibitisha kwamba barua yenye mawasiliano hayo ilikuwa imewekewa stempu ipasavyo na kuandikiwa anwani sahihi, bila kujali kama itakuwa haikuwasilishwa au itarejeshwa bila kuwasilishwa.
(ii) Mteja hatakuwa na madai yoyote dhidi ya Benki kwa madhara yoyote yanayotokana na upotevu, ucheleweshaji, kutokuelewana, uharibifu wa maudhui, urudufu, au kasoro nyingine yoyote inayotokana na uwasilishaji wa mawasiliano yoyote, iwe ni kwenda au kutoka kwa Mteja, Benki au mtu mwingine, kwa njia ya kukabidhi, posta, faksi, telegrafu, simu, teleksi au njia nyingine yoyote ya mawasiliano ya mtandao.
33. Utoaji wa Unafuu
Unafuu au upendeleo wowote utakaotolewa na Benki kwa Mteja hautaathiri wajibu wa Mteja kwa Benki wala haki za Benki dhidi ya Mteja.
34. Usiri
(i) Benki inathamini faragha ya Mteja na ina sera ya kuweka kwa siri taarifa na/au nyaraka zinazomhusu Mteja na/au Akaunti. Hata hivyo, katika mazingira fulani, Benki inaweza kuweka wazi taarifa na/au nyaraka hizo kwa mtu yeyote kuhusiana na tukio la sasa au linalotarajiwa la kushindwa kutimiza wajibu kwa upande wa Mteja. Haki hii ya kuweka wazi inajumuisha pia kuweka wazi taarifa chini ya Vigezo na Masharti haya ya Jumla (ikiwamo uhamishaji au ugawaji wa haki na wajibu wote wa Benki chini ya Vigezo na Masharti haya ya Jumla).
(ii) Mteja anaiidhinisha Benki kujibu, iwapo itaona inafaa, maswali yote (ikiwamo bila ukomo marejeo ya kibenki) yanayopokewa kutoka kwa benki nyingine yoyote, taasisi ya kifedha au mtu yeyote anayetoa mikopo au huduma za kifedha, kuhusiana na Akaunti, bila kumrejea Mteja.
(iii) Benki inaweza pia kuweka wazi taarifa na/au nyaraka zinazohusiana na Akaunti katika mazingira yafuatayo:
- kwa ofisi yoyote ya kumbukumbu za mikopo na kwa benki na taasisi nyingine za kifedha, pamoja na taasisi za usimamizi na tathmini za mikopo;
- kwa mtu yeyote anayetoa taarifa au huduma kwa Benki (ikiwamo bila ukomo kampuni mama au za kundi, kampuni tanzu au wahusika wanaohusiana), kwa masharti kwamba taarifa hizo zitahifadhiwa kwa siri na hazitasambazwa zaidi; na
- pale Benki inapokuwa chini ya wajibu wa kisheria au wa kimkataba kufanya hivyo (ikiwamo bila ukomo wajibu wa kisheria na/au wa kimkataba wa Benki wa kuzuia utakatishaji fedha na makosa yanayohusiana) na/au pale ambapo ni kwa maslahi ya umma.
35. Uhamishaji wa Haki
Benki itakuwa na haki kamili na isiyo na kizuizi ya kuhamisha na/au kukabidhi kwa mtu yeyote haki, manufaa na wajibu wake wote au sehemu yake chini ya Vigezo na Masharti haya ya Jumla na/au chini ya Vigezo na Masharti Mahususi, wakati wowote, bila kutoa taarifa kwa Mteja.
36. Tafsiri
(i) Maneno
“Mteja” na/au
“mtu” na/au
“wahusika” yatamjumuisha mtu binafsi, kampuni, ubia, chombo kilichosajiliwa au cha kisheria, dola, wakala wa dola au mamlaka ya serikali kwa jina au mtindo wowote; na pale ambapo watu wawili au zaidi wamejumuishwa katika neno
“Mteja” na/au
“mtu” na/au
“wahusika”, neno hilo litamjumuisha kila mmoja wao peke yake na/au wote kwa pamoja.
(ii) Marejeo ya maneno yanayoonesha umoja yatachukuliwa kujumuisha wingi na kinyume chake, na marejeo ya jinsi ya kiume yatachukuliwa kujumuisha jinsi ya kike na bila jinsi, na kinyume chake.
(iii) Wajibu wowote unaowekwa au unaotokana na Vigezo na Masharti haya ya Jumla ambao unachukuliwa na zaidi ya mtu mmoja utakuwa ni wajibu wa pamoja na wa kila mmoja, wa kila mtu aliyeuchukua, iwe kama mdaiwa mkuu, mdhamini, mtoaji fidia, au vinginevyo; na
(iv) Kila kifungu cha Vigezo na Masharti haya ya Jumla ni tofauti na kinatenganishwa na vingine. Endapo wakati wowote kifungu chochote cha Vigezo na Masharti ya Jumla kitakuwa kinyume cha sheria, batili au kisichotekelezeka kwa namna yoyote ile, basi uhalali, utekelezekaji na nguvu ya vifungu vilivyobaki haitaathiriwa wala kudhoofishwa kwa sababu hiyo.
37. Marekebisho
(i) Benki inaweza kurekebisha Vigezo na Masharti ya Jumla, Vigezo na Masharti Mahususi yoyote na/au Ada za Benki (kwa ujumla au kwa sehemu) wakati wowote. Taarifa ya marekebisho hayo inaweza kutolewa kwa Mteja kwa maandishi au kwa kuchapishwa kwa njia yoyote itakayoamuliwa na Benki; hata hivyo, marekebisho yoyote, yawe yamearifiwa au vinginevyo, yatamfunga Mteja; na
(ii) Benki inaweza kuanzisha aina mpya ya Akaunti ambayo Vigezo na Masharti Mahususi yatahusika. Endapo kutakuwa na mgongano wowote kati ya Vigezo na Masharti haya ya Jumla na Vigezo na Masharti Mahususi, Vigezo na Masharti Mahususi yatatumika.
38. Mawasiliano ya Fidia
Mteja anakubali kuifidia na kuilinda Benki dhidi ya madai yote, matakwa, hasara, gharama, dosari, dhima na matumizi ya aina yoyote ile (ikiwamo Kodi zozote, ada za kisheria (bili, pale inapofaa, kwa misingi ya wakili/mteja) zinazotumika, matatizo yaliyosababishwa na Benki (au na mtu mwingine yeyote kwa niaba ya Benki) kuhusiana na:
- majadiliano, maandalizi, utekelezaji, utoaji, utozaji stempu au usajili (iwe kwa sehemu au kwa ukamilifu) wa Dhamana yoyote;
- uhifadhi au utekelezaji (au jaribio la kuhifadhi au kutekeleza) wa haki zozote za Benki chini ya au kuhusiana na utekelezaji (au jaribio la utekelezaji) wa Vigezo na Masharti ya Jumla, Vigezo na Masharti Mahususi na/au Dhamana yoyote;
- marekebisho yoyote halisi au yanayopendekezwa, au msamaha wowote kuhusiana na Dhamana yoyote;
- kufutwa au kuachiliwa kwa Dhamana yoyote; na
- miamala yoyote au upatikanaji wa ushauri wa kitaalamu na/au mwingine wowote kuhusu jambo au swali lolote linalotokana au kuhusiana na Vigezo na Masharti ya Jumla, Vigezo na Masharti Mahususi na/au Dhamana yoyote.
39. Sheria Inayotumika
Vigezo na Masharti ya Jumla na Vigezo na Masharti Mahususi yoyote yataongozwa na kutafsiriwa kwa mujibu wa sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Mteja anakubali kuwa chini ya mamlaka ya Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
VIGEZO NA MASHARTI YANAYOSIMAMIA MATUMIZI YA HUDUMA ZA KIDIJITI/KIZAZI KIPYA ZA BENKI YA I&M
1. Ufafanuzi na Tafsiri
1.1 Katika Vigezo na Masharti haya (“Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya”), ikijumuisha Jedwali lolote, isipokuwa kama muktadha utahitaji vinginevyo:
(a)
“Maelezo ya Upatikanaji wa Mfumo” maana yale ni taarifa na/au nyaraka zinazohifadhiwa na Benki kuhusiana na Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa, kwa madhumuni ya upatikanaji wa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa katika Mfumo na/au matumizi ya Huduma.
(b)
“Fomu ya Maombi” maana yake ni fomu inayojazwa kwa ajili ya usajili wa kupatiwa Huduma.
(c)
“Mshirika” maana yake ni ileile kama ilivyofafanuliwa chini ya vifungu vinavyohusika vya Sheria ya Benki na Taasisi za Fedha.
(d)
“Benki” maana yake ni I&M Bank (T) Limited, ikijumuisha (bila ukomo) warithi wake wa kisheria na waliokabidhiwa haki na wajibu (iwe ni kwa uasili wake au kwa kupitishwa), pamoja na Tawi au Kampuni Tanzu yoyote itakayobainishwa na Benki kwa Mteja katika vipindi mbalimbali.
(e)
“Siku ya Kazi za Benki” maana yake ni siku ambayo kaunta za Tawi na/au Kampuni Tanzu (kama itakavyohusika) huwa wazi kwa ajili ya kufanya shughuli za kawaida za kikazi.
(f)
“Tawi” maana yake ni (ikiwamo ofisi kuu iliyosajiliwa ya Benki) maeneo yote, ndani au nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambako shughuli za Benki zinaendeshwa na kufanyika.
(g)
“Akaunti ya Benki” maana yake ni akaunti inayomilikiwa na Mteja katika Benki, ikijumuisha (bila ukomo) akaunti yoyote inayohusiana na mkopo, amana, mkataba, bidhaa, muamala au huduma yoyote iliyoanzishwa na kuendeshwa kati ya Benki na Mteja.
(h)
“Mteja” maana yake ni mmiliki wa Akaunti ya Benki ambaye usajili wake wa Huduma umeidhinishwa na Benki.
(i)
“Akaunti ya Amana” maana yake ni Akaunti ya Benki yenye fedha ambazo Mteja anaweza kuzitoa bila kuwapo kwa kizuizi chochote kutoka kwa Benki.
(j)
“Baruapepe” maana yake ni Barua ya Kielektroniki.
(k)
“Huduma za Kielektroniki za Benki” maana yake ni Huduma ya Benki ya Kidijiti/Kizazi Kipya.
(l)
“Vigezo na Masharti ya Jumla” maana yake ni Vigezo na Masharti ya Jumla yanayohusu Akaunti ya Benki.
(m)
“Huduma ya Kituo cha Simu cha I&M” maana yake ni (ikiwamo bila ukomo) huduma inayotolewa na Benki kwa Mteja ambapo, baada ya maombi sahihi, Mteja anaweza kuzungumza na mwakilishi/wawakilishi walioteuliwa wa Benki kuhusu maswali ya salio la Akaunti ya Benki, miamala katika Akaunti ya Benki, pamoja na kupata taarifa kuhusu bidhaa na huduma za Benki.
(n)
“Huduma Isiyo Rasmi ya I&M” maana yake ni (ikiwamo bila ukomo) huduma inayotolewa na Benki kwa Mteja ambapo, baada ya maombi sahihi, Benki hutuma kwa Mteja baruapepe inayohusika yenye taarifa za salio la Akaunti ya Benki na/au Taarifa ya Akaunti ya Benki na/au taarifa fupi ya miamala sita (6) ya mwisho ya Mteja katika Akaunti ya Benki.
(o)
“Huduma ya IMS ya I&M” maana yake ni (ikiwamo bila ukomo) huduma inayotolewa na Benki kwa Mteja ambapo, baada ya maombi sahihi, Benki hutuma kupitia simu ya mkononi ya Mteja ujumbe mfupi wa maandishi unaoonesha salio la Akaunti ya Benki.
(p)
“Huduma ya Smart Statements ya I&M” maana yake ni (ikiwamo bila ukomo) huduma inayotolewa na Benki kwa Mteja ambapo, baada ya maombi sahihi, Benki hutuma Taarifa ya Akaunti ya Benki kwa Mteja kwa njia ya faksi.
(q)
“Huduma ya Benki ya Kidijiti/Kizazi Kipya” maana yake ni Huduma Isiyo Rasmi ya I&M, Huduma ya IMS ya I&M, Huduma ya
Smart Statements ya I&M na Huduma ya Kituo cha Simu cha I&M, pamoja na huduma nyingine zozote zitakazotangazwa kwa Mteja na Benki katika vipindi mbalimbali.
(r)
“Mtumiaji/Watumiaji Walioteuliwa” maana yake ni mwakilishi au wawakilishi wa Mteja walioteuliwa na kuidhinishwa na Mteja kushikilia na kubadilisha Msimbo wa Namba ya Siri, na hivyo kuingia katika Mfumo na kutumia Huduma kwa niaba ya Mteja.
(s)
“Msimbo wa Namba ya Siri” maana yake ni Namba Binafsi ya Utambulisho ya siri iliyoainishwa katika Fomu ya Maombi, yenye angalau tarakimu sita (6), inayojulikana na Benki, Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa pekee, na ambayo ndiyo kiungo pekee kinachounganisha
Maelezo ya Upatikanaji wa Mfumo.
(t)
“Maombi” maana yake ni maombi au maelekezo yanayopokewa na Benki kutoka kwa (au yanayodhaniwa kutoka kwa) Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa kupitia Mfumo kuhusiana na Huduma, na ambayo Benki, kwa mujibu wa kifungu kidogo cha 4.1, imeidhinishwa kuyafanyia kazi.
(u)
“Huduma” maana yake ni huduma yoyote kati ya Huduma za Kielektroniki za Benki ambazo Mteja ataomba katika vipindi mbalimbali na ambazo Benki itaidhinisha na/au kukubali kuitoa.
(v)
“Kampuni Tanzu” maana yake ni kampuni tanzu moja au zaidi za Benki ambazo Benki inaweza kuzitaja au kuzibainisha kwa Mteja katika vipindi mbalimbali.
(w) “Mfumo” maana yake ni programu ya benki ya vyombo anuwai vya mawasiliano na/au vifaa vinavyomwezesha Mteja kuwasiliana na Benki kwa madhumuni ya Huduma. Pale ambapo upatikanaji kupitia mtandao wa intaneti unahitajika, Mfumo na Huduma, kwa madhumuni ya makubaliano haya, utapatikana kupitia tovuti ya Benki (kwa wakati husika) www.imbank.co.tz.
(x) “Usajili” maana yake ni maombi ya Huduma yanayowasilishwa na Mteja.
1.2 Katika Vigezo na Masharti haya ya Jumla ya Kizazi Kijacho:
(a) Maneno
“Mteja” na/au
“mtu” na/au
“mhusika” yatahusisha mtu binafsi, kampuni, ubia, chombo kilichosajiliwa au cha kisheria, dola, wakala wa dola au mamlaka ya serikali kwa jina au mtindo wowote; na pale ambapo watu wawili au zaidi wamejumuishwa katika maneno hayo, yatahusisha kila mmoja peke yake na/au wote kwa pamoja.
(b) Marejeo ya maneno yanayoonesha umoja yatachukuliwa kujumuisha wingi na kinyume chake; na marejeo ya jinsi ya kiume yatachukuliwa kujumuisha jinsi ya kike na bila jinsi, na kinyume chake.
(c) Wajibu wowote unaowekwa au unaotokana na Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya ambao unachukuliwa na zaidi ya mtu mmoja utakuwa ni wajibu wa pamoja na wa kila mmoja wa kila mtu aliyeuchukua, iwe kama mdaiwa mkuu, mdhamini, mtoaji fidia, au vinginevyo.
2. Usajili wa Mteja
2.1 Baada ya Benki kuidhinisha Usajili wa Mteja na Mteja kulipa ada na tozo kwa Benki, zilizoainishwa katika kifungu cha 7 hapa chini, Benki itampatia Mteja huduma zinazohusika za kibenki kupitia njia za kisasa za mawasiliano, kwa kuzingatia na kwa mujibu wa Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya pamoja na Vigezo na Masharti ya Jumla.
2.2 Endapo Mteja atasajili Huduma Isiyo Rasmi ya I&M, pamoja na Msimbo wa Namba ya Siri, atalazimika kubainisha anwani ya baruapepe katika Fomu ya Maombi; anwani hiyo ya baruapepe itasajiliwa na Benki. Benki itatekeleza Maombi yatakayopokewa kupitia anwani ya baruapepe ya Mteja iliyosajiliwa tu.
2.3 Endapo Mteja atasajili Huduma ya IMS ya I&M, pamoja na Msimbo wa Namba ya Siri, atabainisha namba ya simu ya mkononi katika Fomu ya Maombi; namba hiyo itasajiliwa na Benki. Benki itatekeleza Maombi yatakayopokewa kupitia namba ya simu ya mkononi ya Mteja iliyosajiliwa tu.
2.4 Endapo Mteja atasajili Huduma ya Kituo cha Simu cha I&M, Mteja, pamoja na Msimbo wa Namba, atabainisha ama tarehe yake ya kuzaliwa au tarehe ya kuanzishwa au tarehe ya kusajiliwa (kulingana na hali ilivyo) katika Fomu ya Maombi; tarehe hiyo itasajiliwa na Benki. Benki itatekeleza Maombi yanayohusu Huduma ya Kituo cha Simu cha I&M baada ya tarehe hiyo kuthibitishwa.
2.5 Benki inabaki na haki ya kuongeza, kurekebisha, kubadilisha au kuondoa huduma yoyote wakati wowote, kwa sababu yoyote ile, kwa sharti la kutoa taarifa ya awali kwa Mteja.
3. Vifaa vya Mteja na Majukumu ya Mteja
3.1 Mteja, kwa gharama zake mwenyewe, atatoa na kuweka katika hali salama na bora ya uendeshaji vifaa kama vile kompyuta, programu za kompyuta, simu, mashine ya faksi na vifaa vingine vya mawasiliano pamoja na miundombinu inayohusika (ikiwamo upatikanaji wa mifumo yoyote ya mawasiliano ya umma) na mtandao wowote wa mawasiliano (kwa pamoja “Vifaa”) unaohitajika kwa ajili ya kuingia kwenye Mfumo na kutumia Huduma.
3.2 Mteja atawajibika kuhakikisha utendaji mzuri wa Vifaa, ikijumuisha hasara au ucheleweshaji wowote unaoweza kusababishwa na Vifaa hivyo. Benki haitawajibika kwa makosa au hitilafu zozote zitakazosababishwa na hitilafu ya Vifaa, wala haitawajibika kwa virusi vya kompyuta au matatizo yanayohusiana nayo yanayoweza kutokea kutokana na matumizi ya Mfumo, Huduma na Vifaa. Mteja atawajibika kulipa ada zozote kwa mtoa huduma yeyote anayempa Mteja huduma za intaneti, simu ya mkononi, simu ya kawaida au huduma nyingine zozote za mawasiliano, na Benki haitawajibika kwa hasara au ucheleweshaji unaosababishwa na mtoa huduma huyo.
3.3 Mteja atapata leseni na ridhaa zote zinazohitajika ili kuingia na kutumia Mfumo, na atahakikisha kwamba watu wote anaowaruhusu kuingia kwenye Mfumo wanazingatia sheria na kanuni zote zinazohusiana na matumizi ya Mfumo, na kufuata maelekezo, taratibu na masharti yote yaliyomo katika Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya pamoja na nyaraka zozote zinazotolewa na Benki kuhusiana na matumizi ya Mfumo na Huduma.
3.4 Mteja atazuia upatikanaji au matumizi yoyote yasiyoidhinishwa ya Mfumo na/au Huduma kwa kuhifadhi Msimbo wa Namba ya Siri kwa usiri wakati wote. Mteja atahakikisha kuwa Msimbo wake wa Namba ya Siri haujulikani wala haupatikani kwa mtu yeyote asiyeidhinishwa.
3.5 Mteja atachukua tahadhari zote zinazofaa na zinazohitajika ili kugundua matumizi yoyote yasiyoidhinishwa ya Mfumo na Huduma. Kwa madhumuni hayo, Mteja atahakikisha kuwa mawasiliano yote kutoka Benki yanachunguzwa na kukaguliwa na au kwa niaba ya Mteja haraka iwezekanavyo baada ya kupokewa, ili matumizi au upatikanaji wowote usioidhinishwa wa Mfumo ugunduliwe mapema.
3.6 Mteja atatoa taarifa kwa Benki haraka kwa simu, na kufuatiwa na uthibitisho wa maandishi utakaotumwa siku hiyo hiyo, endapo:
- Mteja ana sababu ya kuamini kwamba Msimbo wa Namba ya Siri yoyote unajulikana au huenda ukajulikana na mtu asiyeidhinishwa na/au uko katika hatari ya kutumika vibaya; na/au
- Mteja ana sababu ya kuamini kwamba matumizi yasiyoidhinishwa ya Mfumo na/au Huduma yamefanyika au yanaweza kufanyika, na/au muamala wowote unaohusiana na Huduma umeingizwa kwa njia ya udanganyifu au Mfumo kutumiwa vibaya.
3.7 Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa hawatatuma wala kujaribu kutuma Maombi yoyote kwa Benki kupitia Mfumo endapo Mteja ana sababu ya kuamini kwamba, kwa sababu yoyote ile, maombi hayo huenda yasipokewe na Benki au huenda yasipokelewe kwa usahihi na kwa kueleweka.
3.8 Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa atafuata wakati wote taratibu za usalama kama zinavyotangazwa na Benki katika vipindi mbalimbali, au taratibu zingine zozote zinazohusika na Huduma kwa wakati unaohusika, hususani zilizoainishwa kwenye tovuti ya Benki au machapisho ya bidhaa. Mteja anakiri kwamba kushindwa kufuata taratibu za kiusalama zilizopendekezwa kunaweza kusababisha ukiukwaji wa usiri wa Maelezo ya Upatikanaji wa Mfumo na kusababisha matumizi yasiyoidhinishwa ya Mfumo na/au Huduma. Hasa, Mteja atahakikisha kwamba Huduma haitumiki, au Maombi hayatolewi, au kazi zinazohusika hazitekelezwi na mtu yeyote isipokuwa mtu aliyeidhinishwa kufanya hivyo.
3.9 Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa hataruhusiwa kuendesha au kutumia Huduma kwa namna yoyote itakayoweza kuiathiri Benki.
3.10 Mteja anaelewa na anakubali kwamba Benki inaweza kuunganisha Akaunti ya Benki yenye watia saini wengi na Maelezo ya Upatikanaji wa Mfumo kwa Mteja na Huduma, pale tu ambapo Mteja amewasilisha kwa Benki Fomu halisi ya Maombi iliyosainiwa na watia saini wote wa Akaunti hiyo ya Benki, ikithibitisha kwamba Benki imeidhinishwa kutekeleza Maombi yote. Itakuwa ni jukumu la Mteja pekee kuhakikisha kwamba hakuna mtu asiyeidhinishwa anayeruhusiwa kutumia Akaunti hiyo ya Benki.
3.11 Benki itakuwa na haki na itaidhinishwa kuitoza Akaunti ya Benki ya Mteja kwa kiasi cha miamala yote iliyotekelezwa kupitia Huduma, pamoja na kutoza Akaunti ya Benki ya Mteja kwa ada zozote zinazohusiana na Huduma kama zitakavyoainishwa na Benki katika vipindi mbalimbali.
4. Mamlaka ya Benki Isiyoweza Kubatilishwa
4.1 Benki inaidhinishwa bila kubatilishwa na Mteja kutekeleza Maombi yote na kumwajibisha Mteja kwa matokeo yake, bila kujali kwamba Maombi hayo hayajatolewa na/au hayajaidhinishwa na Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa, au hayako kwa mujibu wa mamlaka yoyote yaliyopo aliyopewa Mteja. Endapo Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa ataiomba Benki kufuta muamala au maelekezo yoyote baada ya Maombi kupokewa na Benki kutoka kwa Mteja, Benki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, inaweza kufuta muamala au maagizo hayo.
4.2 Benki itakuwa na haki ya kupokea na kutekeleza Maombi yoyote, hata kama Maombi hayo kwa sababu yoyote hayajakamilika au yana utata, iwapo Benki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, itaona kuwa inaweza kutekeleza Maombi hayo licha ya upungufu au utata uliopo katika Mambi hayo.
4.3 Benki haitalazimika kupokea au kutekeleza Maombi yoyote endapo kufanya hivyo kutahitaji upatikanaji, hatua au taarifa kutoka kwa Tawi au Kampuni Tanzu iliyopo katika mamlaka yoyote pale ambapo si Siku ya Kibenki kwa wakati husika ambapo upatikanaji, hatua au taarifa hizo zinahitajika, au endapo kufanya hivyo kutasababisha uvunjaji wa mamlaka yoyote iliyopo, kikomo cha huduma ya mkopo, au makubaliano yoyote yaliyopo kati ya Benki na Mteja. Endapo Benki itapokea au kutekeleza Maombi yoyote kama hayo, Mteja ataendelea kuwajibika na ataifidia Benki dhidi ya madai, matakwa, hasara, gharama, uharibifu, dhima au matumizi yoyote ya aina yoyote ile ambayo Benki inaweza kubeba, kuathirika au kupata kutokana na kupokea au kutekeleza Maombi hayo.
4.4 Endapo kutakuwa na mgongano wowote kati ya masharti ya Maombi yoyote kutoka kwa Mteja na Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya, Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya yatakuwa na nguvu ya kutumika. Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya pamoja na idhini zote na taratibu nyinginezo zinazotokana nayo ni nyongeza ya Vigezo na Masharti ya Jumla na mamlaka nyingine zozote zinazotumika kwa Akaunti ya Benki.
5. Ukomo wa Miamala ya Kielektroniki ya Kibenki
Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa anaweza kuhamisha fedha au kufanya malipo ya kiasi chochote, kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 3.9 cha Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya, ilimradi muamala huo unaohusiana na Huduma hausababishi salio katika Akaunti ya Amana kushuka chini ya kiwango cha salio la chini lililoainishwa kwa Akaunti ya Amana au kuzidisha kiwango cha ukomo cha huduma ya mkopo wa ziada kilichotolewa na kuidhinishwa na Benki kuhusiana na Akaunti ya Amana; isipokuwa pale ambapo Mteja ana Akaunti ya Amana ya Muda Maalumu iliyowekwa dhamana ipasavyo kwa Benki ili kufidia ziada yoyote inayoweza kujitokeza katika vipindi mbalimbali katika Akaunti ya Amana inayohusika. Katika hali hiyo, Akaunti za Amana zinazohusika zinapaswa ziunganishwe katika Mfumo kwa madhumuni hayo, na muamala unaohusika hauwezi kusababisha kiasi cha ziada katika Akaunti ya Amana inayohusika kuzidi kiasi kilichowekwa dhamana katika Akaunti ya Amana ya Muda Maalumu.
6. Taarifa za Miamala na Haki za Mteja Kupata Taarifa Hizi
6.1 Miamala yote inayohusiana na Huduma inayofanywa na Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa mara tu wanaporuhusiwa kuingia katika Mfumo itarekodiwa kwa kipindi chote ambacho Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa anapata Mfumo. Benki itahifadhi nakala za Maombi yote katika muundo unaohusika wa vyombo vingi vya mawasiliano. Aidha, nakala zozote za maandishi za nyaraka zilizoandaliwa na/au kushikiliwa na Benki kwa madhumuni ya kutekeleza muamala kwa mujibu wa Maombi zitaendelea kuhifadhiwa na Benki.
6.2 Nyaraka zote na kumbukumbu nyinginezo za aina yoyote zilizoshikiliwa na/au kutolewa na/au kuhifadhiwa na Benki kuhusiana na Maombi na/au Huduma, pasipo kuwapo kosa lililo wazi, zitakuwa ni uthibitisho kamili wa Maombi na/au Huduma na miamala yote inayohusiana nayo, na hazitakuwa chini ya pingamizi lolote kutoka kwa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa kwa sababu yoyote ile.
6.3 Mteja atachukuliwa kuwa amekubali bila masharti yoyote, na hataruhusiwa baadaye kupinga au kutilia shaka muamala wowote unaohusiana na Maombi na/au Huduma uliomo katika taarifa yoyote ya akaunti iliyotolewa na Benki kwa Mteja kuhusiana na Maombi na/au Huduma, isipokuwa pale ambapo Mteja atawasilisha pingamizi kwa maandishi kwa Benki kuhusiana na miamala hiyo kama ilivyoainishwa katika taarifa hiyo ya akaunti, ndani ya siku kumi na tano (15) kuanzia tarehe ambayo taarifa hiyo ya akaunti ilitolewa au inachukuliwa kuwa imetolewa na Benki kwa Mteja.
7. Tozo
7.1 Mteja atailipa Benki ada ya awali ya kuanzisha huduma na ada ya usajili ya kila mwezi kwa ajili ya Huduma, pamoja na tozo za miamala zinazotumika kwa aina mbalimbali za miamala kuhusiana na Huduma, kama Benki itakavyomjulisha Mteja katika vipindi mbalimbali. Benki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, inaweza kurekebisha tozo na ada hizi baada ya kumpa Mteja notisi ya siku kumi na nne (14) kuhusu marekebisho hayo. Pia, Benki, kwa hiari yake kamili, inaweza kuacha kudai ada za awali za kuanzisha huduma na/au ada za usajili za kila mwezi, au sehemu yake.
7.2 Mteja atalipa kodi yoyote inayotozwa kwa kiasi chochote kinacholipwa na Mteja kwa Benki, pamoja na ada, tozo au ushuru mwingine wowote unaotozwa kwa Mteja au Benki na chombo chochote cha serikali au cha kisheria kuhusiana na utoaji wa Huduma.
7.3 Benki inaidhinishwa bila kubatilishwa, katika vipindi mbalimbali, kutoza kiasi chochote kinachodaiwa kutoka kwa Mteja kwa mujibu wa vifungu vidogo vya 7.1 na/au 7.2 kutoka katika Akaunti yoyote ya Benki ya Mteja, katika fedha yoyote. Mbali na ada zinazolipwa chini ya Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya, tozo na ada zinazotumika kwa Akaunti za Benki ya Mteja pia zitatumika.
8. Kuondolewa kwa Dhima
8.1 Hali Zilizo Nje ya Uwezo wa Udhibiti wa Benki
Benki haitawajibika wala kuwajibishwa kwa hasara yoyote itakayompata Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa endapo Huduma itaingiliwa au haitapatikana kutokana na:
(a) hatua zozote za mgomo au migogoro ya kikazi;
(b) hitilafu au kushindwa kufanya kazi kwa mifumo au vifaa vya Mteja; au
(c) hali nyingine yoyote ile ambayo kwa mantiki ya kawaida iko nje ya uwezo wa udhibiti wa Benki, ikijumuisha bila kikomo, matukio yasiyozuilika, hitilafu, kukatizwa, ucheleweshaji au kutopatikana kwa Mfumo, vitendo vya kigaidi au mashambulizi ya adui, hitilafu za vifaa, kukatika kwa umeme, hali mbaya ya hewa au mazingira ya anga, pamoja na kushindwa kufanya kazi kwa mifumo yoyote ya mawasiliano ya umma au binafsi.
8.2 Malipo ya Bili za Kielektroniki na Uhamishaji wa Fedha
(a) Benki haitawajibika kwa hasara au uharibifu wowote utakaompata Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa kutokana na kuchelewa, kushindwa na/au kukataa kwa Benki kutekeleza Maombi kwa wakati au kabisa, katika mojawapo au zaidi ya hali zifuatazo (kadiri itakavyohusika):
- iwapo Mteja hana kiasi cha kutosha katika Akaunti ya Amana kwa mujibu wa kifungu cha 5 hapo juu;
- iwapo Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa hakuidhinisha malipo ya bili kwa wakati unaotosha ili malipo yafanyike na kuingizwa ipasavyo kwa mlipwaji (mpokeaji wa Mteja) kabla ya muda wa malipo kufika;
- iwapo Mfumo au Vifaa havifanyi kazi kikamilifu;
- iwapo mazingira yaliyo nje ya udhibiti wa Benki, ikijumuisha yale yaliyoainishwa katika kifungu kidogo cha 8.1 hapo juu, yanazuia Benki kufanya malipo au uhamisho;
- iwapo kiasi kilichopo katika Akaunti ya Amana kiko chini ya mchakato wa kisheria, amri ya mahakama au kizuizi kingine chochote kinachokwamisha malipo au uhamisho;
- iwapo Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa hakutoa maelekezo sahihi au kamili kwa malipo au uhamisho, au hakufuata taratibu zilizoainishwa katika Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya au makubaliano mengine yoyote yanayotumiwa na Benki kuhusiana na Maombi ya malipo au uhamisho;
- iwapo Benki ina sababu ya kuamini kuwa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa na/au mtu mwingine yeyote anatumia Huduma kwa madhumuni ya udanganyifu au yasiyo halali;
- iwapo Maombi ya malipo au uhamisho yanahusu kiasi kilichowekwa kwa namna au kwa njia ambayo bado haijakifanya kiasi hicho kupatikana kwa ajili ya utoaji;
- iwapo Maombi ya malipo au uhamisho yanapingana au yanakinzana na makubaliano mengine yaliyopo kuhusiana na Akaunti za Benki.
(b) Endapo Benki itafanya malipo au uhamisho kwa wakati unaofaa lakini mpokeaji atashindwa kuingiza kwa haraka malipo ya Mteja baada ya kuyapokea, Benki haitawajibika kwa hasara au uharibifu wowote utakaompata Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa kutokana na kushindwa huko kwa mpokeaji.
8.3 Fidia
- Mteja ataifidia na kuilinda Benki kikamilifu na bila masharti dhidi ya gharama zote (ikiwamo gharama za kisheria), madai, hatua za kisheria, mashauri, hasara, uharibifu, matakwa, dhima na matumizi ya aina yoyote ile ambayo Benki itapata, kubeba au kuathirika kunakohusiana na au kunakotokana na (a), (b) na/au (c) za kifungu kidogo cha 8.1 pale ambapo mazingira yanayohusika yako chini ya udhibiti wa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa, na pia dhidi ya gharama zote (ikiwamo gharama za kisheria), madai, hatua za kisheria, mashauri, hasara, uharibifu, matakwa, dhima na matumizi yanayotokana na ukiukaji wowote wa masharti yoyote ya hati hii kwa upande wa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa.
- Mteja ataifidia na kuilinda Benki dhidi ya matakwa, madai, hatua za kisheria, hasara, uharibifu, gharama au matumizi ya aina yoyote ile ambayo Benki wakati wowote inaweza kuyabeba, kupata au kuathirika kutokana na utoaji wa Huduma, isipokuwa pale ambapo matakwa, madai, hatua, hasara, uharibifu au gharama hizo zimetokana moja kwa moja na uzembe mkubwa au utovu wa nidhamu wa makusudi wa Benki au wa mfanyakazi yeyote wa Benki.
- Mteja ataifidia na kuilinda Benki dhidi ya yafuatayo:
- madai, mashauri, hasara na uharibifu wa aina yoyote ile unaoweza kuletwa dhidi ya Benki au ambao Benki inaweza kubeba au kupata, unaotokana na utegemezi wa Benki kwa taarifa au data yoyote isiyo sahihi, isiyosomeka, isiyokamilika au isiyo na uhakika iliyomo katika Maombi yoyote;
- hasara au uharibifu wowote unaoweza kutokea kutokana na matumizi, matumizi mabaya, matumizi yasiyo sahihi au umiliki wa programu yoyote ya mtu mwingine na Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa, ikijumuisha (bila ukomo) mifumo ya uendeshaji, programu za kuvinjari au vifurushi vingine vya programu;
- upatikanaji wowote usioidhinishwa wa Akaunti za Benki au ukiukwaji wowote wa usalama, au uharibifu au upatikanaji wa data wowote za Mteja, au uharibifu, wizi au madhara kwa Vifaa vya Mteja;
- hasara au uharibifu wowote unaosababishwa na kushindwa kwa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa kuzingatia masharti na vigezo vinavyotumika kwa Huduma na/au kutokana na kutoa taarifa zisizo sahihi, au hasara au uharibifu unaotokana na kushindwa au kutopatikana kwa mifumo au vifaa vya mtu mwingine, au kushindwa kwa mtu mwingine kushughulikia muamala.
8.4 Endapo, kwa sababu yoyote ile isiyotajwa katika kifungu kidogo cha 8.1, Huduma itaingiliwa au haitapatikana, dhima pekee ya Benki kuhusiana na hali hiyo itakuwa ni kurejesha Huduma haraka iwezekanavyo, au, kwa hiari ya Benki, kumpatia Mteja huduma mbadala za kibenki ambazo si lazima ziwe za kielektroniki.
8.5 Isipokuwa kama ilivyoainishwa katika kifungu kidogo cha 8.4, Benki haitawajibika kwa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa kwa kuingiliwa au kutopatikana kwa Huduma, kwa namna yoyote ile itakavyosababishwa.
8.6 Katika hali yoyote ile, Benki haitawajibika kwa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa kwa hasara yoyote ya faida au akiba inayotarajiwa, wala kwa hasara yoyote isiyo ya moja kwa moja au ya matokeo ya aina yoyote ile, kwa namna yoyote ile itakavyosababishwa, yanayotokana na au kuhusiana na Huduma.
8.7 Isipokuwa kuhusiana na kifo au jeraha la mwili linalosababishwa na uzembe mkubwa au utovu wa nidhamu wa makusudi wa Benki, Benki haitakuwa na dhima kwa dai lolote lolote kuhusiana na Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya au utekelezaji wake, au miamala yoyote iliyotekelezwa na Benki kwa kuitikia maombi yoyote, isipokuwa pale ambapo Benki imepokea notisi ya maandishi ya madai hayo kutoka kwa Mteja kama ifuatavyo:
- kwa madai yoyote yanayohusiana na muamala, ndani ya siku thelathini (30) kuanzia tarehe ya muamala unaodaiwa ambao madai hayo yanategemea;
- kwa madai mengine yote, ndani ya siku tisini (90) kuanzia tarehe ya kitendo au kutotenda kunakodaiwa kwa Benki ambako madai hayo yanategemea.
8.8 Kwa kiwango kinachoruhusiwa kisheria, Benki:
(a) inakanusha dhamana zote zinazohusiana na Mfumo na Huduma, ziwe za wazi au za kudokezwa, ikijumuisha (bila ukomo) dhamana zozote zilizodokezwa zinazohusiana na ubora, kufaa kwa madhumuni maalumu au uwezo wa kufanikisha matokeo fulani;
(b) haitoi dhamana yoyote kwamba Mfumo hauna makosa au kwamba matumizi yake hayatakatizwa, na Mteja anakiri na kukubali kwamba kuwapo kwa makosa hayo hakutachukuliwa kuwa ni ukiukaji wa Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya.
9. Marekebisho
Benki inaweza kurekebisha Vigezo na Masharti haya, ama kwa ujumla au kwa sehemu, wakati wowote, kwa sharti kwamba notisi ya awali au taarifa ya marekebisho hayo itatolewa kwa Mteja kwa maandishi au kwa kuchapishwa kwa njia yoyote itakayoamuliwa na Benki. Marekebisho hayo yatakuwa ya lazima na yatamfunga Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa.
10. Kusitishwa kwa Huduma
10.1 Bila kujali chochote kilichomo katika Vigezo na Masharti haya, Huduma inaweza kusitishwa wakati wowote na Benki au Mteja kwa kumpa mwenzake notisi ya mwezi mmoja wa kalenda. HATA HIVYO, endapo kutatokea mabadiliko yoyote ya sheria au matumizi yake, au tukio lolote ambalo, kwa mtazamo wa Benki, litaathiri au kuleta madhara kwa Benki endapo itaendelea kutoa Huduma kwa Mteja, Benki itakuwa na haki ya kusitisha Huduma haraka bila kutoa notisi kwa Mteja.
10.2 Endapo Mteja atasitisha Huduma, Benki inaweza kuendelea kufanya malipo ya bili za kielektroniki, uhamisho wa fedha na miamala mingine ambayo Mteja alikuwa ameidhinisha hapo awali, hadi pale itakapokuwa imepata muda wa kutosha na unaokubalika wa kuchukua hatua kufuatia notisi ya kusitisha iliyotolewa na Mteja.
10.3 Kusitishwa kwa Huduma hakutasitisha wala kuathiri, kwa peke yake, uhusiano wa Kibenki kati ya Benki na Mteja.
10.4 Vifungu vya 8, 11.3, 11.6 na 12 vitaendelea kuwa na nguvu hata baada ya kusitishwa kwa Huduma.
11. Masharti ya Jumla
11.1 Mteja hataruhusiwa kuhamisha au kukabidhi mafao au haki yoyote inayotokana na Vigezo na Masharti haya bila ridhaa ya awali ya maandishi au uthibitisho kutoka kwa Benki.
11.2 Hakuna msamaha wowote utakaotolewa na Benki kuhusiana na ukiukwaji wowote wa Vigezo na Masharti haya kwa upande wa Mteja na/au Mtumiaji Aliyeteuliwa utakaochukuliwa kuwa halali isipokuwa kama ni msamaha wa wazi uliotolewa kwa maandishi. Msamaha wowote wa ukiukwaji huo hautachukuliwa kuwa ni msamaha wa ukiukwaji wowote wa baadaye.
11.3 Mteja anakiri kwamba:
(a) hajategemea maelezo, dhamana, ahadi, kauli ya maoni au kishawishi chochote kilichotolewa au kudaiwa kutolewa na au kwa niaba ya Benki wakati wa Usajili; na kwamba
(b) hakuna mtu yeyote aliyekuwa au aliye na mamlaka, kabla, wakati au baada ya Usajili, kwa niaba ya Benki, kutoa maelezo, dhamana, ahadi, kauli ya maoni au kishawishi chochote kama hicho kwa Mteja, wala kuingia katika makubaliano yoyote ya pembeni au ya ziada na Mteja kuhusiana na Huduma.
11.4 Vigezo na Masharti haya ya Kidijiti/Kizazi Kipya yanabatilisha makubaliano, mipango na uelewa wote wa awali kati ya wahusika na yanaunda makubaliano kamili na ya mwisho kati ya wahusika kuhusiana na mada iliyomo humu. Kwa kuondoa shaka, hakuna chochote kilichomo humu kitakachobadilisha, kuondoa au kwa namna yoyote kuathiri au kudhuru dhamana yoyote iliyotolewa na Mteja au mtu mwingine yeyote kwa manufaa ya Benki kuhusiana na wajibu wowote wa Mteja unaoweza kutokea endapo Benki itatekeleza Maombi yoyote ya Mteja chini ya Masharti haya.
11.5 Kila kifungu cha Vigezo na Masharti haya ya Kizazi Kijacho ni tofauti na kinaweza kutenganishwa na vingine. Endapo wakati wowote kifungu chochote kitakuwa au kuonekana kwenda kinyume cha sheria, batili au kisichotekelezeka kwa namna yoyote ile, uhalali, nguvu ya kisheria na utekelezekaji wa vifungu vilivyobaki hautaathiriwa wala kudhoofishwa kwa sababu hiyo.
11.6 Notisi yoyote inayotakiwa kutolewa kwa maandishi chini ya Vigezo na Masharti ya Kidijiti/Kizazi Kipya itachukuliwa kuwa imetolewa ipasavyo endapo itatumwa kwa posta iliyosajiliwa, ikiwa imewekewa stempu na kuandikiwa anwani sahihi:
(a) kwa Meneja wa Tawi au wa Benki, kwenye anwani ya posta ya Tawi au ya Benki, endapo itatakiwa kutolewa kwa Benki; au
(b) kwa Mteja, kwenye anwani iliyo katika kumbukumbu za Benki kuhusiana na Akaunti ya Benki, endapo itatakiwa kutolewa kwa Mteja;
na itachukuliwa kuwa imewasilishwa siku tano (5) za kazi za Benki baada ya kutumwa kwa posta.
12. Usiri na Uwekaji Wazi wa Taarifa
12.1 Mteja anakubali kudumisha usiri wa hali ya juu kuhusu Msimbo wake wa Namba ya Siri na taarifa au nyaraka zingine zozote za aina yoyote alizopatiwa na Benki kuhusiana na Huduma. Mteja anakubali kuwajulisha mawakala, wafanyakazi na/au wakandarasi wake kuhusu masharti ya kifungu hiki na kuwawekea wajibu wa usiri huo kupitia mikataba tofauti, pale inapohitajika. Mteja atawajibika kikamilifu kwa Benki kwa ukiukwaji wowote wa kifungu hiki unaofanywa na yeye mwenyewe au na wafanyakazi, mawakala na/au wakandarasi wake.
12.2 Mteja anakubali kwamba, pale itakapohitajika kwa ajili ya utoaji wa Huduma, Benki inaweza kutoa taarifa kuhusu Mteja kwa mshirika yeyote wa Benki au washirika wa Mteja.
12.3 Mteja anakubali pia kwamba Benki inaweza kutoa taarifa kuhusu Mteja kwa watu wengine katika mazingira yafuatayo:
- pale ambapo utoaji huo ni muhimu ili Benki iweze kutekeleza Maombi;
- ili kutii sheria, kanuni, amri ya mahakama na/au wajibu wa kimkataba wa Benki; endapo Benki italazimika kutoa taarifa kwa mamlaka ya serikali iliyoidhinishwa, Benki itamjulisha Mteja kabla ya kutoa taarifa hizo kwa kiwango kinachoruhusiwa kisheria;
- utoaji wa taarifa kwa mawakala, wakandarasi, wakaguzi, mawakili na watoa huduma wengine wa kitaalamu wa Benki, kwa kiwango kinachohitajika katika utekelezaji wa majukumu yao ya kawaida;
- utoaji wa taarifa kwa ofisi ya kumbukumbu za mikopo yenye leseni ambayo Benki imejiunga na huduma zake;
- endapo inahusisha madai ya Benki au dhidi ya Benki kuhusiana na hati iliyowekwa au iliyotolewa dhidi ya Akaunti ya Benki; au
- endapo Mteja ameidhinisha utoaji wa taarifa.
13. Haki za Milki ya Bunifu
13.1 Mteja anakiri kwamba haki za milki ya ubunifu katika Mfumo (pamoja na marekebisho au maboresho yake yoyote yatakayofanyika katika vipindi mbalimbali) na nyaraka zote zinazohusiana nayo ambazo Benki humpatia Mteja kupitia Mfumo au kwa njia nyingine yoyote zinamilikiwa ama na Benki au na watu wengine ambao Benki imepewa haki ya kutumia na kutoa leseni ya Mfumo na/au nyaraka hizo. Mteja hatakiwi kukiuka haki zozote za milki ya ubunifu.
13.2 Mteja hataruhusiwa kunakili, kuiga, au kwa namna yoyote kuhariri au kuingilia Mfumo na nyaraka zinazohusiana nayo bila ridhaa ya awali ya maandishi ya Benki.
14. Sheria Inayotumika
14.1 Vigezo na Masharti haya yataongozwa na kutafsiriwa kwa mujibu wa sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
14.2 Benki na Mteja wanakubali kuwasilisha chini ya mamlaka ya kisheria ya Mahakama za Tanzania, na Benki itakuwa huru kutekeleza uamuzi wowote wa mahakama katika mamlaka yoyote ambako Mteja anafanya shughuli zake au kuwa na mali.
VIGEZO NA MASHARTI YA MATUMIZI YA KADI YA I & M BANK (T) LIMITED
1. FAFANUZI
(a)
“Akaunti” maana yake ni kuhusiana na Kadi, ya akaunti yoyote inayomilikiwa na Mmiliki wa Kadi katika Benki, iwe ni yake peke yake kwa jina la Mmiliki wa Kadi au ni ya pamoja na wamiliki wengine wa akaunti, ambao Benki imewateua kwa maombi ya Mmiliki wa Kadi kuwa akaunti stahiki kwa ajili ya kutekeleza Muamala wa Kadi na ambayo kiasi chote kinachodaiwa kutokana na matumizi ya Kadi kitatozwa katika Akaunti hiyo, isipokuwa pale ambapo Akaunti ni ya pamoja, wamiliki wote wa Akaunti ya pamoja wanapaswa wajaze na kusaini Fomu ya Maombi.
(b)
“Fomu ya Maombi” maana yake ni fomu ya maombi ya Kadi, au maombi yaliyowekwa katika fomu inayohusika iliyojazwa na Mteja kuhusiana na uanzishwaji na uendeshwaji wa Akaunti.
(c)
“ATM” maana yake ni mashine ya kutoa fedha kiotomatiki, iwe nchini Tanzania au kwingineko, ya Benki au ya Mshirika mahususi wa Mtandao wa Pamoja wa Benki, ikijumuisha mtandao wa VISA, ambako Mmiliki wa Kadi anaweza kutekeleza Muamala.
(d)
“Benki” maana yake ni I & M Bank (T) Limited.
(e)
“Kadi” maana yake ni Kadi ya Kutolea Fedha ya “Visa Electron” iliyotolewa na Benki kwa maombi, na kwa jina la Mmiliki wa Kadi kwa matumizi yanayohusiana na huduma za kadi zinazotolewa na Benki.
(f)
“Mmiliki wa Kadi” maana yake ni mtu (iwe mtu binafsi au chombo cha kisheria) ambaye amepewa Kadi na ambaye jina lake limeandikwa kwenye Kadi.
(g)
“Kituo cha Biashara” maana yake ni eneo lililo popote linalokubali Kadi, ikijumuisha (bila ukomo) maduka, migahawa, hoteli au mashirika ya ndege yanayoonesha nembo ya Benki au nembo ya mshirika wa mtandao wa pamoja, ikijumuisha nembo yoyote ya VISA, kama ishara ya kukubali Kadi, na ambako Kifaa cha POS kimefungwa.
(h)
“Namba ya Siri” maana yake ni kuhusiana na Mmiliki wa Kadi, namba binafsi ya utambulisho inayohitajika ili kupata huduma kupitia ATM au Kifaa cha POS kwa ajili ya kutekeleza Muamala.
(i)
“Kifaa cha POS” maana yake ni kifaa cha mauzo kilichowekwa katika Kituo cha Biashara chenye uwezo wa kuchakata Muamala.
(j)
“Mshirika wa Mtandao wa Pamoja” maana yake ni chombo chochote ambacho Benki inaingia nacho makubaliano ambayo, kwa mujibu wake, wamiliki wa kadi ya Benki wanaweza kutekeleza Miamala kwenye ATM na/au Vifaa vya POS vinavyomilikiwa na, au vinavyohusishwa na, chombo hicho; na
“Muamala” maana yake ni muamala wowote unaotekelezwa kwa kutumia Kadi kwa mujibu wa Vigezo na Masharti haya.
2. MATUMIZI YA ATM
(a) Kadi inaweza kutumika kwenye ATM yoyote kwa Miamala ifuatayo:
- kutoza Akaunti kwa kutoa fedha taslimu; na tozo hiyo itafanyika haraka;
- kuingiza katika Akaunti kwa kuweka fedha taslimu au hundi; na uingizaji huo utafanyika ama siku inayofuata ya kazi (kwa amana ya fedha taslimu) au siku ambayo fedha zilizosafishwa zimepokewa;
- kumpatia Mmiliki wa Kadi taarifa fupi ya akaunti;
- kuagiza Muamala mwingine wowote ambao Benki inaweza kuufanya upatikane kwa Mmiliki wa Kadi katika vipindi mbalimbali, ikijumuisha kuongeza muda wa maongezi katika simu na uhamisho wa fedha kati ya akaunti.
(b) Utoaji wote wa fedha taslimu kupitia ATM kwa kila kadi utakuwa chini ya kikomo cha utoaji wa kila siku kama Benki itakavyotangaza katika vipindi mbalimbali, na pia utategemea kuwapo kwa fedha za kutosha katika Akaunti. Mmiliki wa Kadi anakubali kutojaribu kutoa fedha isipokuwa pale ambapo kuna salio la kutosha katika Akaunti. Wajibu wa kuhakikisha kuwa salio la Akaunti linatosha ni wa Mmiliki wa Kadi pekee.
(c) Benki, kwa hiari yake, inaweza kutenga kiwango fulani cha chini kinachopaswa kubaki katika Akaunti; chini ya kiwango hicho, muamala wa kutoa fedha hautaruhusiwa, hata kama kuna fedha za kutosha katika Akaunti kufanya muamala huo. Kiwango hicho kinaweza kubadilishwa na Benki wakati wowote.
(d) Pasipo kuwapo kosa lililo wazi, kumbukumbu za Benki kuhusu Muamala wowote au athari zake zitakuwa uthibitisho kamili.
(e) Mmiliki wa Kadi anapokamilisha Muamala kupitia ATM, anaweza kuchagua kupokea taarifa iliyochapishwa ya Muamala. Hata hivyo, kwa miamala yote ya kuweka fedha/hundi kupitia ATM, Mmiliki wa Kadi anakubali kwamba ATM haitatoa stakabadhi inayoonesha kiasi kilichowekwa; bali itatoa uthibitisho wa kupokea hundi au bahasha (kulingana na hali ilivyo) bila kutaja moja kwa moja kiasi kilichowekwa.
(f) Amana zote za fedha na hundi zitakuwa chini ya uhakiki wa Benki, na kiasi kitakachothibitishwa na Benki ndicho kitakachoingizwa.
(g) Mmiliki wa Kadi anakubali kwamba maombi yanayofanywa kupitia ATM, kama vile maombi ya kitabu cha hundi, yatashughulikiwa siku inayofuata ya kazi.
(h) Mmiliki wa Kadi anashauriwa kuhifadhi taarifa ya Muamala iliyotolewa na ATM.
3. MATUMIZI YA KITUO CHA BIASHARA
(a) Kadi inaweza kutumika katika Kituo chochote cha Biashara. Kadi ni kwa matumizi ya kielektroniki tu.
(b) Baada ya Muamala kuthibitishwa na kuidhinishwa, Muamala utakuwa umekamilika, na hati ya muamala itatolewa na Kifaa cha POS ili ithibitishwe na Mmiliki wa Kadi.
(c) Mmiliki wa Kadi anashauriwa pia kukagua maelezo ya Muamala kabla ya kupokea bidhaa zilizonunuliwa na/au huduma zilizotolewa na kabla ya kuondoka kaunta ya Kituo cha Biashara.
(d) Mara tu Kadi inapochanjwa, kuthibitishwa, na Muamala kuidhinishwa, Akaunti itatozwa haraka thamani kamili ya Muamala.
(e) Benki haitawajibika kwa mipangilio au mazungumzo yoyote ambayo Mmiliki wa Kadi anaweza kufanya na Kituo cha Biashara, ikijumuisha (bila ukomo) aina au ubora wa bidhaa zilizotolewa na/au huduma zilizotolewa, au dhamana zozote zilizotolewa katika Kituo cha Biashara. Endapo Mmiliki wa Kadi ana malalamiko yoyote, yatatatuliwa na Mmiliki wa Kadi moja kwa moja na Kituo cha Biashara. Kushindwa kufanya hivyo hakutamuondolea Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kuhusiana na Akaunti ya pamoja, wamiliki wote wa Akaunti ya pamoja kwa pamoja na kila mmoja) wajibu wowote kwa Benki. Mmiliki wa Kadi anashauriwa pia kuijulisha Benki haraka kuhusu malalamiko, manung’uniko au migogoro yoyote na Kituo cha Biashara.
(f) Benki haitawajibika kwa ada ya ziada yoyote itakayotozwa na Kituo cha Biashara.
(g) Endapo Mmiliki wa Kadi atataka kubatilisha Muamala uliokamilika kutokana na kosa au kutokana na kurejesha bidhaa kwa Kituo cha Biashara, stakabadhi ya awali ya mauzo iliyotolewa na Kituo cha Biashara, pamoja na nakala ya stakabadhi ya kubatilisha, zinapaswa zihifadhiwe na Mmiliki wa Kadi. Urejeshaji/ubatilishaji makato kutokana na miamala hiyo utashughulikiwa kwa njia ya isiyo ya kielektroni na utafanywa na Benki baada ya kupokea nyaraka zinazohusika tu.
(h) Iwapo Mmiliki wa Kadi, au mtu yeyote aliyeidhinishwa kutumia Kadi, atatoa mamlaka iwe kwa kuhusisha kuponi iliyosainiwa, vocha ya usajili, maelekezo ya simu au atatoa namba ya Kadi ili kufanya ununuzi au kupata taarifa ya fedha bila kuwasilisha Kadi (kama vile kwa agizo la barua, agizo la simu au intaneti), athari yake kisheria itakuwa sawa na ile ya Kadi kutumika na Mmiliki wa Kadi na vocha ya mauzo au nyaraka nyingine yoyote (au vocha ya kutoa fedha) kusainiwa na Mmiliki wa Kadi. Benki itaitoza Akaunti ya Kadi kwa kiasi cha miamala yote ya Kadi, na Mmiliki wa Kadi atawajibika kuilipa Benki kiasi chote kilichotozwa, iwe vocha au nyaraka hiyo imesainiwa na Mmiliki wa Kadi au vinginevyo, na bila kujali haki au wajibu wowote kati ya Kituo cha Biashara na Mmiliki wa Kadi.
- KUPOTEA AU KUIBWA KWA KADI AU NAMBA YA SIRI
Mmiliki wa Kadi anatakiwa kuchukua tahadhari zote zinazostahili ili kuhakikisha usalama wa Kadi na Namba ya Siri wakati wote, na kuzuia kupotea na/au matumizi ya Kadi au Namba ya Siri kwa mtu mwingine yeyote. Kwa hiyo, Mmiliki wa Kadi hatakiwi kamwe kumwonesha mtu yeyote Namba yake ya Siri kwa hali yoyote ile.
Iwapo Kadi itapotea au kuibwa, au iwapo Namba ya Siri itaonekana kwa mtu asiyeidhinishwa, Mmiliki wa Kadi anatakiwa kuiarifu Benki haraka kuhusu kupotea, kuibwa au kuonekana huko. Taarifa yoyote ya mdomo inapaswa ithibitishwe haraka kwa maandishi.
Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa Akaunti ya pamoja, wamiliki wote wa Akaunti ya pamoja kwa pamoja na kila mmoja wao) atawajibika kwa Muamala wowote uliotekelezwa kabla ya Benki kupokea taarifa ya maandishi kuhusu kupotea, kuibwa au kuoneshwa kwa Kadi au Namba ya Siri (kulingana na hali itakavyokuwa).
- ADA NA TOZO ZA HUDUMA
Kwa kila Mmiliki wa Kadi, Benki itakuwa na haki, kwa hiari yake kamili na ya pekee, kutoza na kukata katika Akaunti ada na tozo zozote katika vipindi mbalimbali na kumjulisha Mmiliki wa Kadi, ikijumuisha (bila ukomo) ada ya awali ya utoaji wa Kadi, ada ya utoaji upya na/au ubadilishaji wa Kadi, ada ya huduma kwa matumizi ya Kadi kwa kiasi kitakachobainishwa na Benki katika vipindi mbalimbali kwa matumizi ya kadi, na tozo kwa utekelezaji wa Miamala kama Benki itakavyobainisha katika vipindi mbalimbali. Kushindwa kwa Benki kumjulisha Mmiliki wa Kadi hakutaathiri kwa namna yoyote ile haki ya Benki kukusanya ada na tozo hizo kutoka kwa Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, wamiliki wa Akaunti ya pamoja).
Iwapo Kadi itatumika katika ATM zinazomilikiwa na Washirika wa Mtandao wa Pamoja wa Benki, ada ya huduma inaweza kutozwa na mwendeshaji wa ATM na/au mtandao wa uhamishaji wa kielektroniki kwa utekelezaji wa Muamala unaohusika.
- NAMBA BINAFSI YA UTAMBULISHO
Ili kumwezesha Mmiliki wa Kadi kutumia Kadi, Namba ya Siri itatolewa kwa Mmiliki wa Kadi. Namba hiyo ya Siri itatumwa kwa njia ya posta na/au kukabidhiwa kwa Mmiliki wa Kadi baada ya kuthibitishwa kwa utambulisho wake, na Mmiliki wa Kadi atahakikisha kuwa anaipokea katika bahasha iliyofungwa.
Namba ya Siri inaweza kubadilishwa hapo baadaye na Mmiliki wa Kadi, kwa tahadhari zake mwenyewe, kupitia ATM yoyote inayotoa huduma hiyo. Usalama wa Namba ya Siri ni muhimu na unapaswa udumishwe na Mmiliki wa Kadi wakati wote.
Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, wamiliki wa Akaunti ya pamoja, kwa pamoja na kila mmoja wao) anaweza kuwajibika kwa matumizi yasiyoidhinishwa ya Kadi; na maelekezo yoyote yanayotolewa kwa kutumia Kadi na Namba ya Siri, iwe kwa pamoja au kwa kila moja, kwa hiari kamili ya Benki, yanaweza kuchukuliwa kuwa ni maelekezo ya Mmiliki wa Kadi.
Mmiliki wa Kadi atahakikisha kuwa hamwoneshi mtu yeyote Namba ya Siri, na atachukua tahadhari za kutosha kuzuia mtu mwingine yeyote kuiona Namba yake ya Siri ikiingizwa kwenye ATM au Kifaa cha POS. Inashauriwa Mmiliki wa Kadi aikumbuke Namba ya Siri kichwani na afute taarifa zozote zilizoandikwa.
- USALAMA WA NAMBA YA SIRI
Mmiliki wa Kadi anatakiwa:
- kutoonesha Namba ya Siri kwa mtu yeyote, ikijumuisha (bila ukomo) Mmiliki mwingine wa Kadi, mwanafamilia au rafiki;
- kuchukua tahadhari ili kuzuia mtu yeyote kuiona Namba ya Siri ikiingizwa kwenye ATM au Kifaa cha POS;
- kutoandika au kuonesha Namba ya Siri kwenye Kadi au mahali pengine popote, hata kwa njia ya kificho; aihifadhi kichwani na afute taarifa yake yoyote.
- KUREJESHA/KUBADILISHA KADI
Kadi iliyotolewa kwa Mmiliki wa Kadi itabaki kuwa mali ya Benki na inapaswa irejeshwe kwa Benki pale itakapohitajika. Mmiliki wa Kadi anatakiwa kuirejesha Kadi kwa Benki kwa ajili ya kufutwa iwapo hataki tena kuitumia, au endapo Benki, kwa sababu yoyote ile, itaondoa huduma.
Mmiliki wa Kadi hatakiwi kuitumia au kujaribu kuitumia Kadi baada ya kupokea taarifa ya kufutwa au kuondolewa kwa huduma.
Baada ya kupokea maombi ya maandishi ya kubadilisha Kadi iliyoharibika au iliyopotea, Benki, baada ya kufanya uthibitisho unaohitajika, inaweza kutoa Kadi mbadala na kuikata Akaunti kwa ada ya ubadilishaji inayotumika kwa wakati unaohusika.
- USITISHWAJI
Mmiliki wa Kadi anaweza kuacha kutumia Kadi na huduma za kadi ya Benki zinazotolewa na Benki wakati wowote kwa kutoa notisi ya maandishi kwa Benki, ikiambatana na kuirejesha Kadi ikiwa imekatwa vipande viwili.
Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, wamiliki wa Akaunti ya pamoja) ataendelea kuwajibika kwa Miamala na/au ada zote zilizotekelezwa hadi Benki ipokee na kuthibitisha notisi ya maandishi ya usitishwaji.
Benki itakuwa na haki ya kusitisha huduma za kadi ya Benki wakati wowote kwa kuifuta Kadi hiyo, bila kutoa sababu, baada ya kutoa notisi ya siku saba (7). Notisi hiyo itatolewa ama kwa posta kwenda kwenye anwani ya Mmiliki wa Kadi iliyofikia mwisho kwa Benki, au kwa baruapepe kwenye anwani ya baruapepe iliyobainishwa katika Fomu ya Maombi. Notisi itachukuliwa kuwa imetolewa siku saba (7) baada ya kutumwa kwa posta au siku saba (7) baada ya kutumwa kwa baruapepe, kulingana na hali itakavyokuwa.
Baada ya usitishwaji, iwe kwa maombi ya Mmiliki wa Kadi au na Benki, Benki haitalazimika kurejesha kiasi chochote kwa Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, kwa mmiliki yeyote wa Akaunti ya pamoja), iwe ni ada zilizolipwa awali au vinginevyo.
- TAARIFA YA AKAUNTI
Miamala yote inayofanywa kwa kutumia Kadi itaonekana katika Taarifa ya Akaunti ya kila mwezi na itazingatia Vigezo na Masharti ya Jumla yanaiyosimamia Akaunti.
- ADA NA TOZO ZA SERIKALI
Ushuru, ada, kodi au tozo zozote za Serikali au mamlaka nyingine zinazohusika za kodi zinazohusiana na chochote zitalipwa na Mmiliki wa Kadi na kukatwa na Benki katika Akaunti.
- AKAUNTI NA KADI NYINGI
- Kikomo cha utoaji wa fedha cha kila siku kwa Kadi kitahusu jumla ya utoaji wa kila siku unaofanywa kutoka katika Akaunti zote zinazohusishwa na Kadi hiyo.
- Endapo Akaunti ni ya pamoja na mamlaka ni either/or survivor, baada ya kila mmiliki wa Akaunti ya pamoja kujaza na kutia saini Fomu ya Maombi, mmiliki yeyote wa Akaunti ya pamoja anaweza kupewa Kadi inayohusiana na Akaunti hiyo.
- Endapo Akaunti ni ya pamoja na Kadi zimetolewa kwa zaidi ya mmiliki mmoja (au wote) wa Akaunti ya pamoja, kila Kadi itakuwa chini ya kikomo cha utoaji wa fedha cha kila siku kwa Kadi inayohusika.
- GHARAMA ZA UTEKELEZAJI
Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, wamiliki wa Akaunti ya pamoja kwa pamoja na kila mmoja wao) ataifidia Benki kikamilifu na bila masharti kwa gharama zote zitakazotumiwa na Benki katika kutekeleza au kujaribu kutekeleza Vigezo na Masharti haya, au katika kukusanya kiasi chochote kinachodaiwa na Benki kutoka kwa Mmiliki wa Kadi, ikijumuisha ada zote za kisheria, ada za kufungua mashauri mahakamani na matumizi mengine yote.
- MASHARTI YA JUMLA
(a) Kadi haiwezi kuhamishwa na haitakiwi kutumiwa na mtu yeyote isipokuwa Mmiliki wa Kadi.
(b) Kadi itabaki kuwa mali ya Benki, na ikifutwa inapaswa irejeshwe kwa Benki pale inapohitajika.
(c) Kadi iliyotolewa itakuwa na muda maalumu wa uhalali wake, na baada ya muda huo kuisha, Kadi mpya inaweza kutolewa na Benki kwa hiari yake kamili na ya pekee.
(d) Kadi si ya mkopo wala si kadi ya dhamana ya hundi, na Mmiliki wa Kadi hataruhusiwa kuiwasilisha au kuitangaza kama kadi ya aina hiyo.
(e) Akaunti hairuhusiwi kuingia kwenye deni kupitia utekelezaji wa Muamala kwa kutumia Kadi.
(f) Fedha au hundi zinazowekwa kupitia ATM kwa ajili ya kuingizwa kwenye Akaunti zitakusanywa na Benki, na mapato yake hayatapatikana hadi pale Benki itakapopokea fedha zinazohusika kwa thamani kamili.
(g) Utekelezaji wa Muamala wowote utakuwa chini ya masharti au mipaka ya uendeshaji iliyowekwa kwenye Akaunti.
(h) Matumizi ya Kadi yatazingatia kanuni na masharti ya Viza.
(i) Mmiliki wa Kadi anaridhia Benki kufanya uchunguzi kwa madhumuni ya kuthibitisha taarifa zozote zilizotolewa na Mmiliki wa Kadi katika Fomu ya Maombi ya Kadi ya I & M Bank.
(j) Benki inaweza kutoa au kuhamisha haki na mafao yake wakati wowote.
- DHIMA YA MMILIKI WA KADI NA BENKI
(a) Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, wamiliki wa Akaunti ya pamoja kwa pamoja na kila mmoja wao) atawajibika kikamilifu kwa kila Muamala unaotekelezwa kwa kutumia Kadi. Muamala wowote unapaswa utekelezwe kwa namna ambayo haitaweka wazi taarifa za siri zinazoonekana kwenye Kifaa cha POS kwa mtu yeyote mwingine. Benki haitawajibika kwa kuwekwa wazi kwa taarifa yoyote kwa mtu mwingine kunakotokana na utekelezaji wa Muamala.
(b) Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, mmiliki yeyote wa Akaunti ya pamoja) hataiwajibisha wala kuifanya Benki kuwa na hatia kwa namna yoyote dhidi ya hasara, madhara au uharibifu wowote, unaotokana na matumizi ya ATM, ikijumuisha kushindwa kutoa fedha kutokana na ukosefu wa fedha katika ATM ambayo Muamala unafanyika.
(c) Benki haitawajibika kwa kukataa au kushindwa kwa Kituo chochote cha Biashara, Kifaa cha POS au ATM kukubali au kuwajibika kwa Kadi, au kukamilisha Muamala, wala kwa kushikiliwa kwa Kadi na ATM au Kifaa cha POS.
- KWA WAMILIKI WA AKAUNTI WENYE UMRI WA MIAKA 16 HADI 18, KADI YA BENKI INAWEZA KUTOLEWA KWA MASHARTI YAFUATAYO:
(a) Ridhaa ya Mlezi: Utoaji wa kadi ya Benki unahitaji ridhaa ya maandishi iliyo wazi ya mzazi au mlezi wa kisheria.
(b) Kukabidhiwa kwa Mzazi/Mlezi: Kadi ya Benki inapaswa ichukuliwe na mzazi au mlezi aliyetoa ridhaa.
(c) Uwajibikaji: Mzazi au mlezi wa kisheria anayeichukua kadi ya Benki atawajibika kikamilifu kwa matumizi ya Kadi, ikijumuisha mamlaka ya kuamua iwapo amkabidhi mtoto kadi hiyo au aiweke kwa ajili ya uhifadhi salama.
Kwa kukubali masharti haya, mzazi au mlezi wa kisheria anakiri wajibu wake na anakubali kufuatilia matumizi ya kadi ya Benki ya mtoto, na kuhakikisha yanaendana na vigezo na masharti yote yanayosimamia matumizi yake.
- MAZINGIRA YALIYO NJE YA UDHIBITI WA BENKI
(a) Benki haitawajibika kwa kushindwa kutekeleza majukumu yake yanayohusiana na shughuli za ATM kutokana na tukio lolote lililo nje ya udhibiti wa Benki.
(b) Benki haitawajibika endapo itashindwa kutekeleza majukumu yake kutokana na (moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja) kushindwa kwa mashine yoyote, mfumo wa uchakataji wa data au kiungo cha mawasiliano, au migogoro ya kikazi, migomo, kufungiwa kazini, vitendo vya adui wa umma, vita, vizuizi, maasi, ghasia, magonjwa ya mlipuko, maporomoko ya ardhi, radi, matetemeko ya ardhi, moto, dhoruba, mafuriko, machafuko ya kiraia, vitendo vya kigaidi, kanuni na maelekezo ya serikali, au tukio lolote lililo nje ya udhibiti wa moja kwa moja wa Benki, mawakala wake au wakandarasi wake wadogo.
- MAREKEBISHO
(a) Vigezo na Masharti haya yanaweza kurekebishwa na/au kubadilishwa kwa ujumla au kwa sehemu, wakati wowote, na Benki kwa hiari yake kamili na ya pekee. Benki inaweza kumjulisha Mmiliki wa Kadi kuhusu marekebisho na/au mabadiliko hayo; hata hivyo, kushindwa kwa Benki kutoa taarifa hiyo hakutaathiri kwa namna yoyote ile uhalali au utekelezekaji wa Vigezo na Masharti kama yalivyorekebishwa na/au kubadilishwa.
(b) Baada ya marekebisho na/au mabadiliko yoyote ya Vigezo na Masharti haya yatakayofanywa na Benki, matumizi yoyote ya baadaye ya Kadi yatachukuliwa kuwa ni kukubali marekebisho na/au mabadiliko hayo.
- SHERIA
Vigezo na Masharti haya yatatafsiriwa na kutekelezwa kwa mujibu wa sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Mmiliki wa Kadi (na endapo Kadi imetolewa kwa ajili ya Akaunti ya pamoja, wamiliki wote wa Akaunti ya pamoja) anakubali kuwa chini ya mamlaka ya Mahakama Kuu ya Tanzania.